WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO KUBORESHA MKATABA WA HUDUMA KWA WATEJA

Na. Peter Haule, WFM, Arusha

Wizara ya Fedha na Mipango inaboresha Mkataba wa utoaji Huduma kwa wananchi kwa kupata maoni katika maeneo mbalimbali ya utoaji huduma lengo likiwa kuongeza ufanisi na kufikia maendeleo stahiki kwa wakati.

Hayo yamebainishwa na Mchumi Mwandamizi wa Wizara ya Fedha na Mipango Bi. Fortunata Soka, wakati wa mafunzo ya ukusanyaji wa maoni ya maboresho ya Mkataba wa Huduma kwa Wateja   kwa wadau wa Wizara hiyo yaliyofanyika Jijini Arusha na kuwakutanisha wadau kutoka Wizara hiyo pamoja na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Bi. Soka alisema kuwa Wizara ya Fedha na Mipango imekuwa na Mkakati wa Utoaji huduma kwa wananchi ambao sasa unahitaji maboresho ili kuongeza ufanisi wa huduma na kuharakisha maendeleo ya wananchi.

‘’Muundo wa Wizara umebadilika na pia wadau wanaongezeka hivyo kuna kila sababu ya kuboresha mkataba wa huduma kwa wateja ili kukidhi uhitaji, tunalazimika kufanya mafunzo ya namna ya kufanya tafiti kwa wadau ili kuja na mkataba bora uliosheheni weledi na kuleta matokeo chanya kwa walengwa.’’, alieleza Bi. Soka

Alisema kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imejipambanua kwa kufikisha huduma kwa haraka kwa wananchi hivyo  Wizara inalengo la kupata mrejesho wa utoaji wa huduma zake ili kuweza kuandaa mipango yenye manufaa kwa wananchi na Taifa kwa ujumla

Bi Soka alisema kuwa maboresho ya Mkataba wa huduma kwa wateja ni sehemu ya kujali wananchi hasa wa hali ya chini ambao wanataka kupata huduma bora kwa ufanisi kwa maendeleo yao kwa kupunguza urasimu usio wa lazima.

Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi wa Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ambaye pia ni mtoa mada, Bw. Raphael Waida, alisema kuwa ili kuweza kutoa huduma bora kwa wananchi lazima mikataba ya huduma kwa wateja ikafanyiwa maboresho kila inapobidi kwa kuwa teknolojia na mazingira ya kihuduma yanabadilika.

Aidha, ameipongeza Wizara ya Fedha na Mipango kwa jitihada zake za kuhakikisha inatoa huduma kwa wadau kwa wakati hasa katika kipindi hiki ambacho Serikali imejidhatiti kufikia uchumi wa Kati uliojikita katika viwanda kwa manufaa ya wananchi.

Naye Mchumi wa Wizara ya Fedha na Mipango Bw. Henrico Ndagula ambaye ni mmoja wa Washiriki wa Mafunzo amesema kuwa, mafunzo hayo yanasaidia kufanya tathmini ya utoaji huduma na kuangalia maeneo ambayo Wizara imefanikiwa na yanayohitaji maboresho, hivyo kuwa na umuhimu hasa katika wakati huu ambao mabadiliko makubwa yakiuchumi yanafanyika nchini.

Mwisho.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527