WAGOMBEA WANAWAKE WATAKIWA KUTOKATISHWA TAMAA

Kulia ni Diwani wa Kata ya Mshewe Esther Mbega Halmashari ya Wilaya ya Mbeya,kushoto ni Flora Mlowezi.

Na Esther Macha - Malunde 1 blog Mbeya 
Diwani wa Kata ya Mshewe Esther Mbega Halmashari ya Wilaya ya Mbeya Mkoani Mbeya amewataka wanawake wanaogombea nafasi za uongozi uchaguzi wa serikali za mitaa na vijiji kutokatishwa tamaa na baadhi ya wanaume na wanawake wanaodai wanawake hawana sifa za uongozi.

Mbega ameyasema hayo leo wakati wa mafunzo wezeshi kwa wanawake,Vijana na watu wenye ulemavu yaliyoandaliwa na taasisi isiyo ya kiserikali ya TGNP Mtandao yenye lengo la kuwajengea ujasiri kuelekea hatua ya kampeni na uchaguzi.

"Binafsi nilipata vitisho katika uchaguzi mwaka 2015 baadhi wakidai mimi sijaolewa na sijajaliwa kupata mtoto.
Wengine walisema kama mwanamke siwezi kuongoza Kata kubwa kama ya Mshewe ambayo ina changamoto nyingi.

Hata hivyo alisema maneno hayo hayakumkatisha tamaa ambapo alisimama kidete hadi kufanikiwa kushinda kiti cha Udiwani wa Kata ya Mshewe.

ni Naye Mwezeshaji wa mafunzo hayo kutoka TGNP Mtandao Gemma Akilimali aliwataka wagombea kwenda na agenda zinazotekelezeka badala ya kuahidi ahadi zisizotekelezeka.

Gemma alisema wanawake ni wengi na wanazo agenda za kila siku kama ukosefu wa zahanati, maji,miundombinu na uchumi ambazo wakizisemea vizuri zinaweza kuwabeba katika uchaguzi wa serikali za mitaa.

Alisema kitendo cha kuahidi wataleta maji,zahanati wakati hawana pesa bali kwa kushirikiana kwa pamoja wanaweza kuzitatua kwani kiongozi ni muongozaji na mhamasishaji maendeleo na mafanikio yote hupatikana kwa umoja.

Naye Jackson Massawe ambaye pia ni  mwezeshaji wa mafunzo hayo kutoka TGNP Mtandao alisema lengo la TGNP ni kuwajengea uwezo wanawake wanaotarajia kugombea nafasi mbalimbali kupitia vyama vya siasa ili waweze kujiamini kwa kulitawala jukwaa na kujieleza mbele ya wagombea wanaume.

Kwa upande wao washiriki wa mafunzo akiwemo Flora Mlowezi na Felister Kaisi kutoka vituo vya taarifa na maarifa walisema mafunzo hayo yamewaongezea uwezo wa kujiamini.

Mafunzo hayo ya siku tatu yamewapa ari kubwa wanawake hao kuelekea ushiriki wa kampeni na uchaguzi wa serikali za mitaa ambapo wengi wakiomba nafasi ya uenyekiti wa vitongoji vijiji na ujumbe wa halmashauri.

TGNP Mtandao kupitia mafunzo mbalimbali imeleta mabadiliko ya kifikra na kiuchumi ambapo kupitia hoja mbalimbali wanawake wameweza kuiomba halmashauri ya Mbeya kutenga bajeti kwa ajili ya taulo za kike kwa wanafunzi ambao wengi wao kwa mwaka hukosa masomo zaidi ya siku sitini.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527