TPDC YAANZA UTAFITI WA MAFUTA YA PETROL BONDE LA EYASI WEMBERE


Serikali kupitia Shirika la Maendeleo  ya Petroli Tanzania (TPDC) imeanza kufanya utafiti wa mafuta ya petrol katika bonde la Eyasi Wembere ikiwa ni miaka 2 tu imepita tangu Mhe. Rais wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania mhe. Dkt John Joseph Magufuli na Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Museveni walipotia saini makubaliano ya utekelezaji wa ujenzi wa mradi wa Bomba la kusafirisha mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga. 

Utafiti huu unahusisha uchorongaji wa visima vitatu vya utafiti vyenye urefu wa mita 300 kila kimoja na hivyo kufanya jumla ya mita 900 zitakazochorongwa katika Bonde la Eyasi Wembere ambapo Kisima namba moja kinachorongwa katika Kijiji cha Kining’nila Wilaya ya Igunga,kisima namba 2 na 3 vitachoroongwa katika wilaya za Meatu Mkoani Simiyu na Iramba Mkoani Singida. 

Akiongea na waandishi wa habari wakati wa uzinduzi rasmi wa uchorongaji wa kisima namba 1, Meneja utafutaji wa Mafuta na Gesi kutoka TPDC, Bi Venosa Ngowi alisema kuwa utafiti huu unakuja kufuatia ukusanyaji taarifa za bonde hilo uliofanyika mwaka 2015 kwa kutumia ndege maalumu.

 Bi Ngowi alisema baada ya utafiti huo wa kutumia ndege, ulionesha eneo la Bonde la Eyasi Wembere kuwa na miamba tabaka mizuri ambayo inaweza kutumika kwaajili ya utafiti wa Mafuta na gesi hivyo uchorogaji huu wa visima vifupi vya utafiti ni awamu ya pili kufuatia utafiti wa 2015/16. 

Bi Ngowi aliendelea kwa kusema kwamba eneo lote la Bonde la Eyasi Wembere ni muhimu kwaajili ya utafiti huo kutokana na aina ya miamba inayopatikana. 

Akizunguzmia mita zilizochorongwa Katika kisima namba 1 kilichoanza kuchorongwa katika Wilaya ya Igunga amesema tayari zimechoronga mita 116 kati ya 300 zinazopaswa kuchorongwa. 

Nae Meneja Mradi wa Utafutaji Mafuta katika bonde la Eyasi Wembere, ndugu Sindi Mduhu alisema eneo la Bonde la Eyasi Wembere ni kubwa na linaanzia katika Mikoa ya Manyara, Singida,Simiyu, Tabora pamoja na Arusha. 

Baada ya ukusanyaji takwimu za eneoo hilo, kilichofanyika ilikuwa ni kuzichakata na kuzitafsiri ili kuweza kuona ni wapi palio  na miamba tabaka yenye kina kirefu ambacho kianweza kutunza mafuta.

 “Kijiji cha Kining’inila ni mojawapo ya eneo ambalo lilanishwa kama moja ya eneo ambalo uchoroongaji wa visima unaweza kufanyika”. 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Dkt James Mataragio aliyefika ene la utafiti kwaajili ya kujionea kinachoendelea katika utafiti huo alisema utafiti huo unafanyika kwa matumaini kuwa Tanzania inaweza kugundua mafuta. 

“Tunafanya Utafiti kwa kutegemea kwamba kwa kipindi kisichozidi miaka mitano (5) huenda tukagundua mafuta na hivo leo nawadhibitishia watanzania kwamba kazi hiyo inaendelea”. Dkt. Mataragio aliendelea kwa kusema “ kama kule Uganda huenda tukawa na mafuta”. 

Uchorongaji huo utafuatiwa na ukusanyaji wa taarifa za mitetemo ili kuonesha maeneo ambayo yanaweza kuwa na mafuta.

Dkt.mataragio aliongeza kwa kusema kuwa ni nia ya dhati ya Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa  Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kuhakikisha kwamba TPDC si kwamba tu inachimba gesi yake yenyewe bila pia kuhakikisha inagundua mafuta. “ Mhe. Rais angependa kwamba katika kipindi ambacho atakuwa madarakani tuwe tumekwishagundua mafuta kwani tayari tunayo gesi asilia ambayo kwa mwaka 2020 tutaongeza visima vingine ambavyo tutavifanya wenyewe TPDC na sio kwa kutumia wawekezaji kutoka nje ya nchi”.  

Kwa upande wa ushirikishaji makampuni ya ndani katika utafiti huo, Dkt Mataragio alisema kazi yote inafanywa na TPDC kwa kushhirikiana na STAMICO ambalo ni shirika la Serikali na ndiye Mkandarasi Mkuu katika mradi huo. 

Akitaja sifa za maeneo ambayo mafuta yanaweza kugundulika, Dkt.Mataragio alisema ni maeneo ya Bonde la Ufa ambapo kama ilivyo kule nchini Kenya katika eneo la Lokcha au Turkana lipo katika Bonde la Ufa na kule wamegundua mafuta. Vile vile ukienda Uganda Ziwa Albert ambalo lipo katika Bonde la Ufa nao vile vile wamegundua mafuta. 

Kwa upande wa Tanzania, katika eneo la Ziwa Tanganyika ambalo lipo katika Bonde la ufa kuna matonetone ya mafuta hivyo ni dalili nzuri ya uwezekano wa upatikanaji wa mafuta na tayari ukusanyaji wa taarifa za eneo hilo ulikwishafanyika hivyo kitakachofuatia ni ufuatiliaji.

Dkt. Mataragio aliongeza kwa kutaja gharama za mradi wa uchoorgaji visima hivyo mbapo kwa visima vyote vitatu hadi vikamilike vitagharimu fedha za Kitanzania shilingi milioni mia tatu ambapo katika utafiti wa ndege jumla ya shlingi za Kitanzania  shilingi bilioni mbili nukta nne (2.4) zote zikiwa ni fedha za ndani na Serikali.  

Mwenyekiti wa Kijiji cha Kining’inila Christopher Njilezengo ambapo ndipo utafiti huo unafanyika, aliipongeza Serikali kwa kukubali kuwekeza katika mradi huo kwani utakuwa na tija kwa taifa endapo utafanikisha upatikanaji wa mafuta. 

“Tunaishukuru sana Serikali kupitia TPDC kwani tunaamini ya kwamba wanatekeela sera ya chama cha mapinduzi chini ya uongozi shupavu wa Mhe. Rais Magufuli ambapo asingekuwa yeye basi mambo hayo wasingeyaona”. 

Bi. Neema Masanja mkazi wa Kijiji cha Kining’inila ambapo ndipo utaifit uanfanyika aliiipongeza Serikali kwa utafiti huo na kunonesha matumaini makubwa katika utafiti unaofanyika na endapo mafuta yatapatikna. “ Mafuta yakipatikana itawezesha upatikanaji wa fursa mbalimbali kwa wanachi ili kuleta maendeleo katika Kijiji chetu na taifa”. 

Tayri baadhi ya wanachi wa Kijiji hicho wameanza kuonja neema ya utafiti huo ambao kuna baadhi yao wamepatiwa kazi mbali mbali zisizohitaji elimu kubwa kama vile upishi, ulinzi pamoja na vibarua. 



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527