RAIS MUSEVENI AINGILIA KATI MAANDAMANO YA WANAFUNZI WA MAKERERE....AYAAGIZA MAJESHI KUONDOKA CHUONI MARA MOJA


Rais wa Uganda, Yoweri Museveni ameagiza wanajeshi wanaozingira chuo kikuu cha Makerere kwa lengo la kutuliza maandamano waondoke mara moja chuoni hapo kwani hiyo sio kazi yao na badala yake jeshi la polisi lisimamie ulinzi chuoni hapo.

Wiki iliyopita, Wanafunzi 15 walikamatwa na Polisi kwa kuchochea vurugu na maandamano wakipinga ongezeko la asilimia 15 ya karo chuoni hapo.

Kwenye maandamano hayo wanafunzi hao walichoma vituo viwili vya Polisi mjini Kampala, Jambo lililopelekea Jeshi liingilie kati ili kutuliza ghasia hizo.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa mapema wiki hii na Afisa Habari wa Rais Museveni, Don Wanyama amesema kuwa Museveni ameagiza Wanajeshi waondoke chuoni hapo na jukumu hilo lichukuliwe na Jeshi polisi.

“Rais Museveni kasema wadau na viongozi wa chuo cha Makerere wakae chini kujadili matatizo yanayoendelea katika chuo hicho. Asubuhi hii amempigia Mkuu wa Chuo kamwambia wakae na wenzao wajadiliane. Pia ameagiza Wanajeshi waondoke chuoni hapo na kazi hiyo iwe chini ya Jeshi la Polisi la Uganda,”amesema Wanyama.

Mpaka sasa hatma ya ongezeko la ada chuoni hapo bado haijapatikana, Lakini hali ya usalama imeanza kurejea.

Ongezeko la 15% liliidhinishwa na baraza la vyuo vikuu nchini Uganda, Wanafunzi wanatakiwa kuanza kulipa ada yenye ongezeko hilo kwa miaka mitano ijayo baadaye kila mwanafunzi atatakiwa kulipa 75% zaidi.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527