NAIBU WAZIRI WA MADINI ATEMBELEA ENEO LENYE MGOGORO WA WACHIMBAJI WADOGO


Serikali imeingilia kati mgogoro uliodumu kwa muda mrefu katika eneo la wachimbaji wadogo lililopo katika Mlima wa Sakenke kata ya Misigiri Wilaya ya Iranga Mkoani Singida.

Mgogoro huo uliodumu kwa takribani miaka 3 ni kati ya mchimbaji mdogo aliyekuwa afisa usalama  wa taifa mstaafu John Lutebeka, na Nabii Elia wote wanagombea eneo hilo ambalo Lutebeka anamiliki ardhi ya juu na Elia ameliombea Leseni ya Uchimbaji Madini.

Akizungumza kwenye eneo linalogombewa, Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo, amewataka Lutebeka, Nabii Elia na Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Singida, Chone Malembo wafike ofisini kwake Jijini Dodoma siku ya Jumatano Oktoba 16 mwaka huu kwa ajili ya kutatua mgogoro huo na kila mmoja aje na vielelezo vinavyomruhusu kuchimba madini katika eneo hilo.

Aidha, Nyongo amewataka Maafisa Madini kote Nchini kutoa elimu kwa wachimbaji juu ya sheria za madini ili kuepusha migogoro isiyo ya lazima maana kuna haki ya umiliki wa ardhi ya juu na kuna haki ya umiliki wa ardhi ya chini kwa maana ya leseni ya uchimbaji hawa wote wana haki sawa wanaweza wakakaa wakazungumza  wakachimba pamoja.

Wakati huo huo Naibu Waziri Nyongo, amemtaka Nabii Elia aachane na uchimbaji wa madini karibu na nguzo za umeme anatakiwa awe mita 100 kutoka kwenye nguzo za umeme, vinginevyo atachukuliwa hatua.

Pia nyongo amewapongeza wachimbaji wa madini wa Mkoa wa Singida kwa ulipaji mzuri wa kodi na amesema rasilimali ya madini ni ya Watanzania wote, hatuko tayari kumuoneo mtu wala hatakubari mtu achimbe amdhulumu mwingine.

“Kwenye uchimbaji kuna kelele nyingi, kuna wengine wanamiliki leseni nyingi hata kuzihudumia hawawezi, mpaka sasa tumefuta leseni elfu 13 hivyo wale wanaojua wasitumie ujuaji wao kuwadhuru wengine tutampa haki mwenye haki yake,” alisema Nyongo.

Awali Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Singida, Malembo, alisema kwa nyakati tofauti, ofisi yake imesuluhisha  mgogoro huo, lakini Lutebeka huwa haridhiki na maamuzi tunayofikia ikabidi tuligawe eneo hilo leye hekari 7.2 na kumpa Lutebeka hekari 4 lakini bado hakuridhika.

Akizungumza kwa  masikitiko, Mkuu wa Wilaya ya Iramba Huhahuka amesema anasikitika kuingizwa kwenye mgogoro huo ambapo Afisa Usalama wa Taifa Mstaafu Lutebeka amekuwa akimtuhumu kuwa anawadhamini hao wanaotaka kuchimba eneo hilo.

Kwa mujibu wa Afisa Madini Mkazi wa Singida, Malembo amesema, kati ya Julai na Oktoba 11 mwaka huu, wamekusanya mapato ya zaidi ya shilingi 1.3 bilioni, Mapato hayo ni sawa na asilimia 271.94 ya lengo  kwa awamu ya kwanza la kukusanya shilingi 500,000,000, na asilimia 90.65 ya lengo la mwaka la kukusanya shilingi 1,500, 000,000/=.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527