UJERUMANI, UFARANSA, UHOLANZI ZASITISHA MAUZO YA SILAHA KWA UTURUKI BAADA YA KUIVAMIA KIJESHI SYRIA


Ujerumani haitaidhinisha tena mauzo ya silaha  ambazo zinaweza kutumika katika mashambulizi ya kijeshi ya Uturuki kaskazini mwa Syria, waziri wa mambo ya kigeni Heiko Maas ameliambia gazeti la Bild am Sonntag.

"Kutokana  na mashambulizi  ya  kijeshi  ya  Uturuki kaskazini mashariki  mwa Syria , serikali  ya shirikisho haitatoa  tena vibali vipya  kwa  ajili  ya  vifaa  vya  kijeshi  ambavyo vinaweza  kutumika na  Uturuki nchini  Syria," Maas  amesema.

Maas  aliongeza kwamba  serikali  ya  Ujerumani  tayari imeweka vizuwizi katika  mauzo ya  nje ya  silaha  zake  kwa  Uturuki katika mwaka  2016 kutokana  na  mashambulizi  ya  nchi  hiyo katika  jimbo la  Afrin.

Washirika  wa  mataifa  ya  magharibi wamekosoa operesheni  ya Uturuki ndani  ya  Syria, ambayo  ilianza siku  ya  Jumatano , ikisema inatishia  mzozo  mkubwa  wa  kibinadamu pamoja  na  kufufua  kundi la itikadi  kali la  Kiislamu  linalojiita  Dola  la  Kiislamu  katika  eneo hilo.

Siku  ya  Jumamosi , wizara ya  mambo  ya  nje  na  ulinzi mjini  Paris zilisema  kuwa  Ufaransa  inasitisha  mauzo  yake  ya  silaha  kwa Uturuki  kutokana  na  mashambulizi  ya  Uturuki kaskazini  mwa Syria.

Serikali  mjini  Paris imeamua  kusitisha  mipango  yote ya  mauzo ya  silaha  kwa  Uturuki  ambayo  inaweza  kutumiwa  katika mashambulizi, wizara  hizo zilisema  katika  taarifa  ya  pamoja.

Siku  ya  Ijumaa , Uholanzi ilisema  imesitisha  kwa  muda mauzo yake  ya  silaha  kwa  Uturuki, na  Sweden  ikasema itatafuta kuungwa  mkono kwa  ajili  ya  kuwekewa  vikwazo  vya  Silaha Uturuki  na  mataifa  yote  ya  Umoja  wa  Ulaya katika  mkutano  wa mawaziri  wa  mambo  ya  kigeni  wa  Umoja  huo wiki  ijayo.

-DW


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527