ALIYEKUWA MKURUGENZI WA MIPANGO, UFUATILIAJI NA TATHIMINI WA TAKUKURU AOMBA MSAMAHA NA KUKIRI MAKOSA YAKE KWA DPP

Aliyekuwa Mkurugenzi wa Mipango, Ufuatiliaji na Tathimini wa TAKUKURU, Kulthum Mansoor amemuandikia barua Mkurugenzi wa Mashtaka nchini(DPP) kwa ajili ya kukiri makosa yake .

Mansoor anakabiliwa na mashtaka manane ya kughushi, kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na kutakatisha Sh.Bil 1.477.

Hayo yamebainika baada ya Wakili wa Serikali Mwandamizi, Wankyo Simon kumueleza Hakimu Mfawidhi, Kelvin Mhina wa kuwa bado upelelezi wa kesi haujakamilika.

Baada ya kueleza hayo, Wakili wa Utetezi, Elia Mwingira amedai kuwa wameandika barua kwenda kwa DPP kwa ajili ya kuomba msamaha na kukiri makosa hivyo ni vyema kupata majibu kwa haraka ili mshtakiwa aweze kupata haki yake ya msingi.

“Tunaomba upande wa mashtaka kulifuatilia hili ili mteja wetu aweze kupata haki yake ya msingi,” alidai Mwingira.

Baada ya maelezo hayo Wakili Simon amedai kuwa suala hilo atalifuatilia kwa haraka zaidi.

Hakimu Mhina ameahirisha shauri hilo hadi Oktoba16, 2019 itakapokuja kwa ajili ya kutajwa.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527