WAZIRI WA KILIMO WA TANZANIA MHE JAPHET HASUNGA AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA WAZIRI WA KILIMO NA MAENDELEO VIJIJINI WA ISRAEL

Na Mathias Canal, Bet Dagan-Israel

Waziri wa Kilimo wa Tanzania Mhe Japhet Hasunga (Mb) tarehe 5 Septemba 2019 amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Kilimo na Maendeleo Vijijini wa Israel Mhe Uri Yehuda Ariel HaCohen na kukubaliana kwa kauli moja kuwa serikali za nchi hizo mbili kuingia makubaliano ya kuendeleza kilimo hususani katika utafiti, Tija katika uzalishaji, na Teknolojia.

Katika mkutano huo uliohudhuriwa pia na Balozi wa Tanzania nchini Israel Mhe Job Daud Masima, Mhe Hasunga ametoa shukrani kwa Serikali ya Israeli kuipatia Tanzania nafasi 100 za kujifunza kuhusu sekta ya kilimo kwa vijana kupitia programu inayosimamiwa na Agrostudies.

Waziri Hasunga ameeleza katika mkutano huo dhamira ya Serikali ya Tanzania inayoongoza na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt John Pombe Magufuli, ya kuwasaidia vijana waliorudi nyumbani baada ya mafunzo hayo kwa kuanza kuwapatia mahitaji ya msingi ikiwemo ardhi ambayo ipo eneo litakalowawezesha kujiendeleza.

Vilevile ameeleza kuwa katika wizara ya kilimo hakukuwa na kitengo cha masoko hivyo ili kuwaunganisha vijana hao na masoko ya biashara watakazozalisha serikali ya Tanzania kupitia wizara ya Kilimo imeanzisha kitengo maalumu cha kushughulikia masoko ya mazao mbalimbali ya wakulima.

Waziri Hasunga pia amezungumzia kuhusu maeneo yanayoweza kuwavutia wawekezaji kutoka Israeli ili kuwekeza nchini Tanzania kwa kutoa takwimu za ukubwa wa ardhi yenye rutuba, uwepo wa maji na hali ya hewa inayoruhusu ukuaji wa aina nyingi ya mazao.

Serikali ya Israeli ipo tayari kusaini hati ya makubaliano ya kilimo (Memorandum Of Undarstanding-MOU) ya kilimo pale itapowasilishwa na Serikali ya Tanzania, hii imekuja baada ya Mheshimiwa Waziri Hasunga kuona umuhimu wa kuingia makubaliano ili iwe rahisi wawekezaji kutoka Israel kuzuru Tanzania kuwekeza pamoja na kupata mikopo kutoka katika Serikali yao.

Akizungumza kwa niaba ya Serikali ya Israeli Waziri wa Kilimo na Maendeleo Vijijini wa nchi hiyo Mhe Uri Yehuda Ariel HaCohen imehaidi pindi Serikali ya Tanzania itakapowasilisha mahitaji hasa kwenye mazao ambayo muhimu ya kuanza nayo kwa ajili ya soko la Israel itakuwa tayari kushirikiana kwa kutoa ujuzi pamoja na uwezeshaji wa wataalamu.

Hata hivyo itakapotokea mwekezaji wa Israeli ataposhirikiana na kampuni ya Tanzania, Serikali inawajibu kuingilia kati kusaidia maeneo ya uwezeshaji na rasilimali watu.

MWISHO


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527