MPANGO KAZI WA TAIFA WA KUTOKOMEZA UKATILI DHIDI YA WANAWAKE NA WATOTO WAJADILIWA

NA.MWANDISHI WETU

WADAU wa masuala ya Wanawake na Watoto wamekutana ili kujadili na kufanya tathimini ya Utekelezaji wa Mpango Kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto (MTAKUWWA) kwa kipindi cha robo ya kwanza 2019/2020.

Akizungumza wakati akifungua kikao kazi hicho cha siku mbili kuanzia Septemba 18 hadi 19, 2019 kilichofanyika katika Ukumbi wa Bwalo la JKT UMWEMA mkoani Morogoro Mratibu wa Taifa wa Mpango huo Bi. Happiness Mugyabuso amesema, Serikali kwa kushirikiana na Washirika wa Maendeleo wameandaa kikao kazi hicho ili kujadili na kufanya tathimini ya utekelezaji wa Mpango Kazi huo.

 “Leo tumekutana hapa kwa pamoja kwa lengo la kufanya tathimini ya utekelezaji wa mpango kazi huo katika kipindi cha robo ya kwanza kwa Mwaka 2019/2020. Aliongezea kuwa, pamoja na mafanikio yaliyopatikana katika robo ya kwanza ya utekelezaji wa Mpango Kazi, kikao kazi kitajadili pia changamoto zilizojitokeza katika kipindi husika na kuweka mikakati mahsusi ya kuimarisha utekelezaji wake kwa vipindi vya robo zinazofuata,”alisema Bi. Happiness.

Aidha kikao hicho kilitoa fursa ya kujadili namna bora ya kuboresha mfumo wa ukusanyaji na uchakataji wa taarifa za takwimu za utekelezaji wa MTAKUWWA ili kuimarisha upatikanaji wa takwimu za msingi (baseline data). Hatua hii ni muhimu kwani itasaidia kupima hali ya utekelezaji wa Mpango Kazi katika vipindi mbalimbali vikiwemo vya mwaka na miaka mitano (5).

Mmoja wa washiriki wa kikao hicho Bw.Emmanuel Burton ambaye ni Afisa Maendeleo ya Jamii kutoka Idara kuu ya Maendeleo ya Jamii alieleza kuwa, Miongoni mwa maeneo yaliyojadiliwa ni pamoja na namna bora ya upatikanaji wa taarifa sahihi za utekelezaji katika sekta mbalimbali ambazo zinatekeleza mpango huo na kuwa na mikakati ya namna ya kuwafikia walengwa kikamilifu ili kukidhi lengo mpango ifikapo mwaka 2021/ 2022.

“Kikao kazi hiki ni muhimu kwa kuzingatia kuwa, malengo mahsusi ya utekelezaji wa Mpango wa MTAKUWWA yanajadiliwa na kuhakikisha tunaandaa taarifa sahihi zenye tija kuhusu makundi hayo ili vita dhidi ya ukatili wa wanawake na watoto inapiganwa na kuleta matokeo chanya,”alisema Burton

=MWISHO=


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527