MKURUGENZI APEWA SAA NNE KUSITISHA MKATABA WA UJENZI


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ametoa muda wa saa nne kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Iringa Himid Njovu awe ameandika barua ya kusitisha ujenzi wa ukumbi wa mikutano na sherehe katika eneo la shule ya msingi Gangilonga.

Amesema maeneo yote ya taasisi za elimu nchini hayaruhusiwi kujengwa miradi ambayo haihusiani na masuala ya elimu, hivyo amtaka mkurugenzi huyo kusitisha mkataba na mtu aliyemkodisha eneo hilo na kisha alizungushie uzio kwa matumizi ya shule.

Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo (Jumamosi, Septemba 28, 2019) wakati akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Iringa, Halmashauri ya Manispaa ya Iringa na Madiwani wa Halmashauri hizo akiwa katika siku ya tano ya ziara yake ya kikazi mkoani Iringa.

“Mkurugenzi kafute mikata yote ya ujenzi wa miradi katika eneo la shule ya Gangilonga pamoja na shule ya Wilolesi kwa sababu maeneo hayo hayaruhusiwi kujengwa miradi isiyohusiana na elimu. Eneo hilo lisafishwe na ujengwe uzio.”

Kwa upande wake, Mwanasheria wa Manispaa ya Iringa Nocholous Mwasungura amesema aliandaa mkataba wa kupangisha eneo kwa maelekezo ya Kamati ya Fedha, ambapo Waziri Mkuu alimuuliza kwa nini hakuwashauri kuhusu suala hilo kwa sababu tayari Serikali ilishatoa waraka wa kuzuia jambo hilo.

Pia, Waziri Mkuu amemwagiza Mkuu wa Mkoa wa Iringa Ally Happi ofisi ya ardhi ya Manispaa ya Iringa kutokana na kuwepo kwa malalamiko mengi kutoka wananchi juu ya Afisa Ardhi ambaye anadaiwa kujigawia viwanja vingi pamoja na kugawa kiwanja kimoja kwa mtu zaidi ya mmoja.

Awali, Mkuu wa Mkoa wa Iringa Ally Happi aliwaonya watumishi hao kutojihusisha na vitendo vya rushwa na matumizi mabaya ya madaraka pamoja na kuacha chuki, ubinafsi na roho mbaya na badala yake washikamane na wafanye kazi wa bidii.

Naye,Mkuu wa wilaya ya Iringa, Richard Kasesera aliiomba Serikali izisaidie halmashauri za wilaya hiyo vyombo vya usafiri kwa sababu magari mengi ni chakavu hali inayosababisha Mkurugenzi wa Manispaa awe anaomba lifti kwake. Waziri Mkuu amewataka waombe kibali cha ununuzi wa magari na watumie fedha zao za ndani.

 (mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527