UBORESHAJI DAFTARI LA WAPIGA KURA KUFANYIKA OKTOBA 2 HADI 8, 2019 KAGERA



Kamishina wa Tume ya taifa ya uchaguzi Mhe. Asina Omari  akizungumza kwenye mkutano wa wadau wa uchaguzi mkoani Kagera uliofanyika katika ukumbi wa Manispaa ya Bukoba.
Kaimu mkurugenzi Daftari na Tehama Frank Mhando akizungumza kwenye mkutano wa wadau wa uchaguzi mkoani Kagera uliofanyika katika ukumbi wa Manispaa ya Bukoba.


Na Lydia Lugakila - Malunde 1 blog 

Tume ya Taifa ya Uchaguzi imesema imekamilisha maandalizi ya zoezi la Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura mkoani Kagera unaotarajia kufanyika kwa siku 7 kuanzia Oktoba 2 hadi 8,2019.


Hayo yamesemwa leo na Kamishina wa Tume ya taifa ya uchaguzi Mhe. Asina Omari  wakati akizungumza kwenye mkutano wa wadau wa uchaguzi mkoani Kagera uliofanyika katika ukumbi wa Manispaa ya Bukoba.


Omari ameeleza kuwa tayari tume imefanya uhakiki wa vituo vya kujiandikisha, uandikishaji wa majaribio, maandalizi ya vifaa vya uboreshaji wa daftari , mkakati wa elimu ya mpiga kura na uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura.

Amesema kutokana na kakamilika kwa mchakato huo,uboreshaji huo utafanyika kwa kutumia Teknolojia ya kielekroniki ya Biometriki (BVR) na kuwa uboreshaji wa safari hii haitahusisha wapiga kura wote waliojiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapiga kura mwaka 2015.



"Uboreshaji huu utawahusisha wapiga kura wapya ambao wametimiza umri wa miaka 18 na wale ambao watatimiza umri wa miaka 18 siku ya uchaguzi mkuu wa mwaka ujao (2020), na pia ambao wamehama maeneo yao ya wali na kuhamia maeneo mengine ya uchaguzi na waleambao kadi zao zimeharibika au kupotea wanatakiwa kuondolewa kwenye daftari kama vile waliofariki na waliopoteza sifa",amesema.

Bi Omary amesema kuwa mchango wa wadau wa uchaguzi hao ni mkubwa katika kupambana na changamoto mbalimbali ikiwemo mila potofu katika jamii hasa zile zinazozuia ushiriki wa baadhi ya makundi ya watu hususani wenye ulemavu.

Kwa upande wake Kaimu mkurugenzi Daftari na Tehama Frank Mhando amewahimiza wananchi kutunza kadi zao vizuri  na kutoa taarifa sehemu husika pale vinapojitokeza vitendo vya uvunjifu wa amani.

Mhando amesema wadau wa uchaguzi wahakikishe wanazingatia sheria taratibu na kanuni na kuwa zoezi la uboreshaji wa daftari hilo hautafanyika katika maeneo ya maficho bali utafanyika sehemu za wazi.


Nao wadau hao kwa pamoja wameahidi kutekeleza zoezi hilo kwa kufuata sheria kanuni na taratibu za nchi.

Picha ya pamoja na wadau wa uchaguzi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527