Tukio la ajabu limetokea katika kijiji cha Maji Mazuri, eneobunge la Lugari kaunti ya Kakamega nchini Kenya baada ya jamaa kumwandalia kuku wake mazishi.
Joseph Victor Omulai alisema ni kweli alimpenda kuku wake sana na alimuuma kumpoteza Septemba 19,2019.
Katika hafla hiyo, mdaku wetu anatuarifu kuwa, jamaa huyo aliimba nyimbo za kuomboleza,kupiga muziki nyimbo za maombolezo usiku, na hata kumwaga machozi kabla ya kusoma vifungu fulani katika Biblia kabla ya kumzika kuku huyo.
Aliongeza kuwa ni lazima atamwandalia makumbusho siku za usoni. “Nilinunua kuku saba na wengine waliibwa na nikabaki na huyu mmoja ambaye sasa ni marehemu. Alikuwa na mayai 12, na nilikuwa nasubiri yaanguliwe vifaranga lakini kwa bahati mbaya, mtu alimpiga na kumuua,” Omulai alisema huku akifuta machozi.
Anasema alimlisha kuku wake mapema kabla ya kuondoka kwenda kusaka mkate wa kila siku lakini aliporejea alimpata kuku wake akiwa marehemu. “Ni uchungu kaka yangu, siwezi kuamini rafiki yangu amekufa," aliongeza kusema.