KAILIMA: NIMERIDHISHWA MAENDELEO YA UJENZI JENGO LA UHAMIAJI DODOMA


Na Mwandishi Wetu-MOHA, Dodoma
NAIBU Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Ramadhani Kailima, ameridhishwa na maendeleo ya ujenzi wa jengo la ghorofa 8 la Idara ya Uhamiaji Makao Makuu, linalojengwa Mjini Dodoma.


Ujenzi huo utagharimu sh. bilioni 30 na unatarajiwa kukamilika Novemba, 2020 ila unaweza kumalizika kabla ya muda huo kama hakutatokea changamoto yoyote.

Kailima aliyasema hayo jana alipofanya ziara ya kujionea maendeleo ya ujenzi huo.

Jengo hilo linajengwa na Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la
Kujenga Taifa (SUMA JKT).

Alisema ziara hiyo imelenga kutekeleza maelekezo ya Rais Dkt. John Magufuli juu ya kuhamia Dodoma.

Alifafanua kuwa, SUMA JKT ina Wakandarasi wazuri wenye uzoefu mkubwa kwenye ujenzi wa majengo mbalimbali.


“SUMA JKT unapowapa mradi, ujenzi wake huwa unakamilika kwa wakati ndio maana hupewa kazi nyingi za ujenzi wa majengo ya Serikali,” alisema.

Kailima alisema hadi sasa ujenzi umekamilika kwenye hatua ya awali (chini), lengo la Serikali ni kuifanya Idara ya Uhamiaji
iondokane na uhaba wa majengo kwenye mikoa mbalimbali.

“Hivi sasa tunaendelea na ukarabati kwenye majengo ya Uhamiaji Mtwara, Lindi, ukarabati mwingine utafanyika Manyara,” alisisitiza Kailima.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527