SALMA AHUKUMIWA JELA MIAKA 99 DAR


Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es salaam imemhukumu kifungo cha miaka 99 jela Salma Mntambo baada ya kupatikana na hatia katika mashtaka 17 ikiwemo kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu.

Miaka hiyo 99 inatokana na makosa 14 ya kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu ambapo kwa kila kosa amehukumiwa miaka sita jela, huku katika makosa matatu ya kutoa nyaraka za uongo kila kosa amehukumiwa miaka mitano jela.

Hukumu hiyo imesomwa  jana Septemba 18, 2019 na  Hakimu Mfawidhi Kelvin Mhina wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Mhina alisema, Mahakama kupitia mashahidi watano waliolioletwa na upande wa mashtaka wameweza kuthibitisha pasipo kuacha shaka kuwa mshtakiwa ametenda kosa hilo.

Hata hivyo Hakimu Mhina amesema adhabu hizo zitaenda pamoja hivyo mshtakiwa  atakaa gerezani kwa miaka sita tu. 

Pia Mahakama imesema kuhusu suala la fidia atatafakari na kufanya utafiti ili aje kutoa oda ambayo ni sahihi hivyo Oktoba 2, mwaka huu atatoa oda hiyo ya fidia

Katika kesi hiyo, mshtakiwa huyo alikuwa akikabiliwa na mashtaka 24 hata hivyo ametiwa hatiani katika mashtaka 17 yakiwamo ya kutakatisha fedha jumla ya Sh. 1.027,000,000 kutoka kwa Ridhuan Mringo huku akijua fedha hizo zimetokana na zao la makosa tangulizi ya kugushi, kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na kuwasilisha nyaraka za uongo.

Katika kosa la kugushi,  mshtakiwa Mntambo anadaiwa kati ya June mosi 2003 na Oktoba 31, mwaka 2011 maeneo yasiyojulikana Wilayani Ilala, mkoani Dar es Salaam kwa nia ya udanganyifu aligushi risiti yenye namba 001226 ya tarehe 10/06/2003 ili kuonesha kwamba Ridhuan Mringo alinunua nyumba ya Shirika la Nyumba iliyopo Plot namba 710 mtaa wa Mfaume Upanga kwa Sh. Millioni 70 wakati akijua ni uongo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527