Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametumia dakika moja kuwaombea dua majeruhi na watu waliopoteza maisha yao kwenye ajali ya moto iliyotokea leo asubuhi katika eneo la Msamvu- Mkoani Morogoro.
Akitoa salamu za pole kabla ya kuanza hotuba ya ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa mwaka wa Shirikisho la Wanafunzi wa Elimu ya Juu nchini (Tahliso) unaofanyika katika ukumbi wa Nkuruma, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) leo Jumamosi, Majaliwa amesema ajali hiyo inasikitisha.
"Mpaka sasa kuna majeruhi zaidi ya 63 hali zao sio nzuri sana, tunawaombea kwa Mungu ili wapone haraka. Ajali hii imetokana na lori na ndugu zetu hawa walienda kujipatia mafuta," amesema Majaliwa.
Akizungumzia mkutano huo, Majaliwa amesema amani na utulivu vilivyopo kwenye vyuo vya elimu ya juu nchini vinaonyesha kuna watu wanatekeleza wajibu wake ipasavyo.
Amempongeza Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako na taasisi zilizo chini ya wizara hiyo kwa kuendelea kutatua changamoto zinazowakabili wanafunzi wa elimu ya juu.
Social Plugin