WANAKIJIJI ZAIDI YA 200 WAUA MIFUGO NA KUICHOMA MOTO KAGERA



Katika hali isiyo ya kawaida na ya kuogofya, takribani wanakijiji zaidi ya 200 wa kijiji cha Kishanda B Wilaya ya Kyerwa Mkoani Kagera, wamevamia shamba la mwananchi mwenzao kisha kuikatakata migomba yote, kuchinja mifugo huku mbuzi wengine wakiwaua kwa kuwachoma na moto.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera Ahmed Msengi, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza vitu vilivyoharibiwa ni pamoja na mashamba ya migomba, kahawa na miti pamoja na kuwaua mbuzi wanne na kuwajeruhi mbuzi wawili, huku chanzo cha mgogoro huo ni umiliki ardhi kubwa, mgogoro ambao tayari ulishafika mahakamani.

Tukio hilo lilifanywa wakati mwenye shamba na mifugo iliyoharibiwa, Tryphone Jeremiah akiwa katika ibada kanisani na kudai kwamba wananchi hao takribani 200, walivamia mashamba na mifugo hiyo saa 6:00 mchana, baada ya kuwepo mgogoro wa ardhi baina ya baba yake na wanakijiji hao tangu mwaka 2007.

"Wananchi wanalalamika kuwa ninamiliki ardhi kubwa, baada ya wanakijiji hao kuvamia mashamba kwa makundi makundi, waliyafyeka kwa muda fupi na kuua mbuzi na kuwachoma moto pamoja na kubomoa nyumba," alidai Jeremiah.

Inaelezwa kuwa wananchi hao walitumia takribani masaa matatu kutekeleza unyama huo na kwa mujibu wa mlalamikaji (Jeremiah), anasema alikuwa na mbuzi 100, hivyo kati ya wale waliochinjwa na waliobaki hai wanaonekana 39 na mbuzi 57 hawaonekani kabisa.
Chanzo - EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527