WANANCHI MWALO WA RUBAFU WAILILIA SERIKALI IWAJENGEE VYOO

Na Lydia Lugakila - Malunde1 blog Bukoba
Wananchi waishio katika Mwalo wa Malehe uliopo katika kata ya Rubafu Halmashauri ya wilaya ya Bukoba mkoani Kagera wameiomba serikali kuwajengea vyoo ili kuepukana na msongamano wanaokumbana nao wakati wa kupata huduma ya kujihifadhi.


Wananchi hao wametoa kero hiyo leo Agosti mosi 2019 katika mkutano wa kusikiliza kero za wananchi ulioandaliwa na ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo  ambapo wamesema , kutokana na wakazi kuongezeka kila kukicha huduma ya choo imekuwa kero na kutokidhi mahitaji yao.

Wamesema kwa sasa wana choo kimoja tu chenye matundu 6 matatu yakiwa ni ya wanaume na matatu ya wanawake ambapo choo hicho hushindwa kuhimili wingi wa watu huku kukiwa na mchanganyiko wa watu wazima na watoto suala ambalo linaweza kupelekea kutokea kwa magonjwa mbalimbali ya mlipuko.

"Katika mwalo huu tupo wengi wengine huingia na wengine hutoka, sisi kama wananchi tulitumia nguvu zetu kujenga choo hiki, sasa hakina uwezo wa kutuhudumia sisi na familia zetu, tunaomba serikali itujengee choo kingine ili kuepusha uchafuzi wa mazingira", alisema mmoja wa wananchi hao.

Aidha kero zilizoibuliwa na wananchi hao ni pamoja na kutopata huduma ya afya kwa saa 24 kutoka katika kituo cha Zahanati Kyamalange, kuvamiwa  na kupigwa  na wanajeshi wa nchi jirani ya Uganda kwa kile walichodai kuwa ni kutojua mipaka ya ziwa na kujikuta tayari wameingia  kwenye maji ya nchi hiyo, kunyangan'ywa mazao yao ya samaki na watu wanaosadikika kuwa ni askari polisi pamoja na uhaba wa miundo mbinu katika shughuli zao.

Akijibu kero hizo kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Dkt. Themistocles Kamugisha amesema serikali kupitia Halmashauri ina mpango wa kupanga  makazi ya mwalo huo na kuwalasimisha na hapo ndipo watakapoweza kuwajengea choo kingine ambacho ni bora na imara baada ya kuachana na makazi holela yaliyoko pembezoni mwa ziwa.

Kuhusu,kero ya kuvamiwa ziwa wanajeshi wa nchi jirani ya Uganda,Themistocles amesema kero hiyo ni kubwa hivyo ataifikisha kwa mkuu wa wilaya ambaye ndiye mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama wa wilaya hiyo ambaye anaweza kuja na kuwaonyesha wavuvi hao mpaka ndani ya ziwa hilo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527