WAHUNI WADUKUA AKAUNTI YA TWITTER YA MWANZILISHI WA TWITTER

Wadukuzi walichukua kwa muda udhibiti wa akaunti ya Twitter ya mwanzilishi na mkurugenzi wa mtandao wa kijamii wa Twitter.

Kundi la wadukuzi linalojiita Chuckling Squad limedai kuhusika na udukuzi wa akaunti ya Twitter ya Jack Dorsey.

Akaunti hiyo iliyo wa mashabiki zaidi ya milioni nne ilianza kutumiwa kusambaza taarifa za chuki na kibaguzi kwa kutumia lugha chafu kwa karibu dakika kumi na tano.

Twitter inasema mitambo yake haikufikiwa na wadukuzi na badala yake kulaumu kampuni ya mawasiliano ambayo haikutaja jina lake kwa kusababisha hitilafu hiyo.

"Nambari ya simu inayohusishwa na akaunti hiyo ilivamiwa kutokana na hitilafu ya kiufundi iliyosababishwa na kampuni hiyo ya mawasiliano ," ilisema taarifa iliyotolewa na Twitter.

"Hali hiyo ilitoa fursa kwa watu wasio na idhini ya kutumia nambari hiyo kuanza kutuma ujumbe kwenye mtandao wa Twitter."

Chanzo cha habari kutoka Kampuni hiyo ilithibitishia BBC kuwa wadukuzi walitumia mfumo unaojulikana kama "simswapping" kuchukua udhibiti wa akaunti ya Twitter ya Bw. Dorsey.

Huu ni mfumo ambao inatumiwa kuhamisha nambari halisi ya simu ya Dorsey katika laini nyingine- na kuanza kuitumia.

Wadukuzi mara nyingine hutoa hongo kwa wahudumu wa kampuni za mawasiliano au kuwapotosha kupata namabari halisi.

Kwa kuchukua udhibiti wa nambari hiyo wadukuzi waliweza kuandika ujumbe moja kwa moja katika akaunti ya Twitter ya Bw. Dorsey.

Japo siku hisi watumiaji wengi wa mtandao huo wanatumia programu tumishi kwenye simu zao kutuma ujumbe, awali Twitter ilibuniwa katika mfumo wa kutuma ujumbe mfupi- hali inayoisaidia kudhibiti idadi ya maneno mtumiaji anastahili kuandika.

Wadukuzi waliandika nini?

Ujumbe wa chuki na wa kibaguzi - ulitumwa moja kwa moja kwa kutumia akaunti ya @jack, na wengine wakasambaza ujumbe huo kwa kutumia akaunti zingine.

Ujumbe mmoja uliashiria kuna bomu limetegwa katika makao makuu ya kampuni hiyo.

Chuckling Squad imedai kuhusika na udukuzi wa Twitter za watu mashuhuri,kama vile mwanablogu wa masela ya urembo James Charles miongoni mwa watu wengine.

Japo tukio hilo linaonekana kufanyika nje ya kampuni hiyo, linasalia kuwa aibu kwa mtandao wa kijamii wa Twitter, unaotoa huduma kwa viongozi wenye nguvu zaidi ulimwenguni.
Chanzo- BBC

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527