SERIKALI YAJIPANGA KUONGEZA USHIRIKIANO NA SEKTA BINAFSI


Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Dar es salaam
Serikali imesema kuwa imejipanga lkuongeza ushirikiano na Sekta binafsi  katika kuhakikisha kuwa kero na vikwazo vinaondolewa ili kuweka mazingira bora ya biashara na kuvutia uwekezaji wa ndani na nje ya nchi.

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) ameyasema hayo leo tarehe 24 Agosti 2019 wakati akimuwakilisha Waziri Mkuu Mhe Kassim Majaliwa kufungua Mkutano mkuu wa mwaka wa dharura wa TCCIA mwaka 2019 huku akiongeza kuwa serikali imefanya uamuzi mahususi mwaka huu wa kuondoa muingiliano wa utoaji wa huduma za mashirika ya TBS na TFDA ili kupunguza usumbufu kwa Wanyabiashara.

Alisema kuwa hizo ni hatua za awali na ametoa mwito kwa TCCIA kuhakikisha kuwa wafanyabiashara wanafuata sheria, kanuni na taratibu zote zilizowekwa ili kuondoa usumbufu wote unaoweza kujitokeza wakati wa kufanya biashara.

Alisema kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt John Pombe Magufuli alizindua  Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Kilimo (ASDP II) tarehe 4 Juni, 2018. Kwa kutambua umuhimu wa Sekta Binafsi, moja ya maboresho makubwa ya ASDP II ukilinganisha na ASDP I ni kuipa nafasi kubwa zaidi Sekta Binafsi.


Aliongeza kuwa ni wakati muafaka wa kubaini maeneo maalumu ambayo Taasisi hiyo ya TCCIA itaendelea kutoa mchango mkubwa katika kutekeleza programu hiyo ili iweze kufikia malengo yaliyowekwa.


Mhe Hasunga amesema kuwa ili kuhakikisha uboreshaji wa Mazingira ya biashara nchini, Serikali kwa kushirikiana na Sekta Binafsi iliandaa andiko maalumu “Blue Print” ambalo lilikwisha zinduliwa, pia mpango wa utekelezaji wake umeandaliwa na umeanza kutekelezwa.


“Ni wajibu sasa wa kila pande yaani Sekta ya Umma na Binafsi kuhakikisha kuwa yale yote yaliyoainishwa katika andiko hilo yanatekelezwa ipasavyo” Alikaririwa Mhe Hasunga


Vile vile, amesema kuwa serikali imeendelea na jitihada za kuimarisha Mabaraza ya Biashara ya Mikoa na Wilaya ambapo tayari imeshaweka Mwongozo wa Mabaraza hayo ambayo TCCIA ni Sekretarieti.


Waziri Hasunga amewataka washiriki hao kuchangamkia  fursa zilizopo katika miradi mikubwa inayotekelezwa na Serikali nchini, hasa miundo mbinu ya reli ya Kisasa, mradi wa umeme wa bwawa la Nyerere, barabara za kisasa, bomba la mafuta, manunuzi ya ndege n.k.


Alisema kuwa Fursa hizo kwa kupitia sera ya “Local Content” nao wakiwa wazawa wana nafasi kubwa ya kunufaika nazo.


Amesema, Miradi hiyo ni mingi na itachukua muda mrefu ikitekelezwa kwa awamu tofauti. “Endapo kwa sababu moja au nyingine haukuweza kupata fursa ya kushiriki kazi kwenye mradi mmoja kwa sababu fulani zikiwemo sifa kadhaa basi, nakushauri ujipange vizuri kwenye miradi inayokuja, msikate tamaa” Alisisitiza Mhe Hasunga


Alisema kuwa serikali inatambua ushirikiano mzuri wa TCCIA na taasisi mbali mbali za Umoja wa Mataifa (UN) zikiwemo UNDP, UNIDO, FAO, UNV, UNESCO, ILO, na ITC, pamoja na Wadau wengine wa kimaendeleo kama Trade Mark East Africa.

Ushirikiano huo kwa kupitia mifumo ya kielektroniki ya kuripoti na kufuatilia vikwazo mbalimbali (NTBs Reporting and Monitoring System) na utoaji wa vyeti vya Uasili wa Bidhaa kwa njia ya kielektroniki (Electronic Certificates of Origin) umesaidia sana uondoaji wa vikwazo vya biashara visivyokuwa vya kiforodha (NTBs).

Pia, TCCIA imeshirikiana na Wadau wengine kama vile VSO, ENGEN, USAID, East African Trade Hub, BMZ, KOICA, JICA, TRIAS na DANIDA kupitia Local Investment Climate (LIC) kuimarisha biashara na mfumo wa majadiliano na sekta ya umma. Kwa kipekee ninawapongeza sana kwa mashirikiano hayo.

MWISHO


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527