MAAFISA MIPANGO WAHIMIZWA KUSHIRIKIANA NA IDARA ZA AFYA KUJUA MIRADI INAYOFADHILIWA NA UNICEF

Na Amiri kilagalila-Njombe

Idara za maafisa mipango zilizopo kwenye halmashauri za wilaya nchini zimetakiwa kupata ushirikiano wa karibu na Sekta ya afya ili kusaidia kutokwamishwa kwa jitihada za shirika la kuhudumia watoto Unicef.

Wito huo umetolewa na wadau wa afya na lishe kutoka mikoa ya Iringa,Mbeya,Songwe na Njombe lli kufikia lengo la kulinda afya ya mama na mtoto.

Mratibu wa asasi zisizo za kiserikali kutoka ofisi ya Rais tawala za mikoa na serikali za mitaa (Tamisemi), Dennis Londo wakati wa ufunguzi wa kikao cha wadau wa masuala ya afya na lishe kilichofanyika halmashauri ya mji Makambako mkoani Njombe amesema  maafisa mipango wengi wamekuwa hawafahamu kinachoendelea kuhusu miradi inayofadhiliwa na Unicef na badala yake taarifa sahihi zinafichwa.

“Ni vibaya kiasi ambacho DED kama accounting officer anaonekana kama mgeni katika miradi yake yeye mwenyewe,afisa mipanga ambaye ndio mkono wa DED katika kumuelezea mipango na utekekelezaji,changamoto na mafanikio, mara nyingi amekuwa hafahamu nini ambacho kinatokea hasa kwenye miradi ambayo inafadhiliwa na Unicef”alisema Dennis Londo

Afisa lishe wa Unicef, Abraham Sanga amesema wanaendelea kushirikiana na serikali katika kufuatilia fedha zinazotolewa  kuona zinawafikia walengwa hasa watoto ambao ndiyo walengwa.

“Tunashirikiana na serikali katika kufuatilia na  kuhakikisha fedha zinazotolewa zinawafikia walengwa hasa watoto kwa hiyo sisi kwa upande wetu tunaufuatiliaji huo wa mara kwa mara”alisema Abraham Sanga

Jachinda Chang’a  ni afisa mipango na uratibu ofisi ya mkoa wa Njombe  na  Theresia Yomo ni afisa ustawi wa jamii mkoa wa Njombe ambao kwa nyakati tofauti wameelezea manufaa yaliyopatikana katika mkoa wa Njombe kupitia ufadhili wa Unicef  huku wakikiri kuwepo kwa changamoto za ufuatiliaji wakati wa mipango.

“Wadau wetu wamekuwa wakituwezesha,katika sekta hizi lakini kumekuwa na changamoto mbali mbali za ufuatiliaji wakati wa mipango,na hili tumejipanga kuliboresha,hata hivyo sisi wataalamu tunapaswa kutathmini tumefanya kazi kwa kiwango gani na ni wapi ambapo palikuwa na gape”alisema Jachinda Chang’a


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527