AFUNGWA JELA MAISHA KWA KUNAJISI MTOTO KAHAMA



Na Salvatory Ntandu - Malunde 1 blog Kahama
Mkazi wa kijiji cha Kakola wilayani Kahama mkoani Shinyanga, Majaliwa Chrisant amehukumiwa kifungo cha Maisha jela na Mahakama ya wilaya ya Kahama baada ya kupatikana na hatia ya kumlawiti/kunajisi mtoto mwenye umri wa miaka 10.

Hukumu hiyo imetolewa Agosti 28,2019 na Hakimu mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo Evodia Kyaruzi na kusema kuwa Mahakama imeridhika na ushahidi uliotolewa na upande wa Jamhuri ambao umethibitisha pasipo shaka yeyote kuwa alitenda kosa hilo.

Amesema Mahakama imepitia ushahidi wa pande zote uliotolewa katika shauri hilo na kubaini kuwa Majaliwa alitenda kosa hilo na kutoa adhabu hiyo ya kifungo cha maisha jela ili iwe fundisho kwake na kwa watu wengine kwenye jamii.

Kyaruzi amesema kosa hilo lina adhabu kali kwa mujibu wa sheria hivyo ametoa ovyo kali kwa watu wengine kwenye jamii wanaowalawiti watoto kwa makusudi na kusema kuwa ukipatikana na hatia katika kosa hilo utafungwa maisha jela.

Kabla ya kutolewa kwa hukumu hiyo Majaliwa aliiomba Mahakama impunguzie adhabu kwani ni kosa lake na kwanza na ana familia inayomtegemea hoja ambayo imetupiliwa mbali na Mahakama hiyo.

Awali akisoma shauri hilo la jinai namba 389 la mwaka 2018 mwendesha mashitaka wa Jeshi la Polisi Felix Mbisse amedai Mahakamani hapo kuwa Majaliwa alitenda kosa hilo kinyume na kifungu 154 (1)(a) na (2) sura 16 ya kanuni ya adhabu kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Majaliwa Tayari ameshaanza kutumikia kifungo cha maisha jela na rufaa yake ipo wazi ndani ya siku 60 kama hajaridhika na hukumu hiyo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527