ZITTO KABWE AMTAKA WAZIRI JAFFO KUSIMAMIA UCHAGUZI WA SERIKALI ZA MITAA KWA HAKI


Kiongozi wa Chama Cha ACT- wazalendo na Mbunge wa Kigoma Mjini Mh.Zitto Kabwe, amemtaka Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi),Mh.Selemani Jafo kusimamia uchaguzi wa Serikali za Mitaa na kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa mujibu na taratibu zilizowekwa pasipo kukiuka utaratibu ili wananchi waweze kumchagua kiongozi wao ambaye watamchagua.

"Natoa wito kwa Waziri wa Tamisemi, Jafo ahakikishe kwamba uchaguzi wa serikali za mitaa unafanyika kwa uhuru na haki. Tunataka wananchi wakachague viongozi wanaowataka na siyo kuvuruga uchaguzi, hilo hatutakubali," amesema Zitto.

Ameyasema hayo leo akiwa anafungua matawi 10 ya chama hicho akisindikizwa na mshaurii wa chama hicho Bw. Seif Sharif Hamad pamoja na viongozi wengine wa chama hicho katika kata ya Vingunguti jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na wananchi wa kata ya Vingunguti Jijini Dar es Salaam, amesema kuwa mkakati ambao wameupanga ni kuhakikisha masuala ya haki na uchumi unakuwa katika hali ya kuridhisha hapa nchini.

Aidha Zitto amesema kuwa lengo ni kuhakikisha kata ya Vingunguti kuongozwa na viongozi wa ACT-Wazalendo hivyo ameviomba vyama na visitumie mabavu katika Uchaguzi ujao ili kuweza kutenda haki kwa wapiga kura na wananchi kwa ujumla pasipo bughudha


Kwa upande wake, Maalim Seif amewataka vijana kusimama imara katika kutetea demokrasia hapa nchini kwa sababu wao ndiyo nguvu kazi ya Taifa hili na wanaweza kuleta mabadiliko wanayoyataka.

Mwanasiasa huyo mkongwe amewataka vijana kufikiria kesho yao kwa kuleta mabadiliko chanya ambayo yataleta maendeleo katika Taifa hili. Amewataka wawe jasiri kupigania demokrasia na maendeleo ya nchi yao.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527