SERIKALI YAJIPANGA KUZUIA MBU WAAMBUKIZAO HOMA YA DENGUE


Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amewataka waganga wakuu wa mikoa kuchukua hatua za makusudi kuzuia mbu waambukizao homa ya dengue na kusisitiza mikoa iliyo mpakani kuchukua tahadhari ya ugonjwa wa ebola.

Waziri Mwalimu ameagiza hayo jana jijini Dodoma wakati akifungua mkutano kikao kazi cha viongozi mbalimbali wa hospitali za rufaa za mikoa.

Alisema waganga wakuu ambao maeneo yao yamekumbwa na ugonjwa wa homa ya dengue na hata mikoa ambayo haijakumbwa na tatizo hilo kuhakikisha wanaangamiza mazalia kwa kutumia dawa ya viuadudu.

“Ninachotaka kusisitiza kwa waganga wakuu, najua wenzetu katika wilaya na halmashauri wanaweza wasituelewe, lakini lazima tuchukue hatua za kudhibiti mbu, hakuna maajabu mengine ambayo tutayafanya zaidi ya kudhibiti mbu.

“Kwa hiyo zile lita chache tunazowapa za dawa kuna wengine wanaona muda unaenda wanaenda katika mito wanazimwaga, hapana, lazima tukafanye kazi ya kunyunyuzia katika mazalia ya mbu,” alisema Ummy.

Alisema mashine hizo zitasambazwa katika baadhi ya mikoa ambayo ina mazalia na kuwataka waganga wakuu kuwabana wakurugenzi watenge bajeti kwa dawa hizo.

“Kipekee nimpokeze Mganga Mkuu wa Dar es Salaam amepambana sana na bahati nzuri Katibu Tawala wake amemshika vizuri, nasema kwamba ukipewa majukumu lazima ufanye kazi.

“Tanga sijaona jitihada zozote kukabiliana na dengue, nasema kweli kwa sababu mimi natoka Tanga ila watu wanaumwa, Pwani angalau kidogo,” alisema.

Kuhusu ugonjwa wa ebola, alisema Serikali inaendelea kuchukua hatua za kukabiliana nao kama utatokea huku akiupongeza Mkoa wa Mwanza kwa jinsi ulivyojiandaa kuukabili.

“Ebola bado ni tishio nchini, nilitoa taarifa kwa umma, lakini hakuna ‘case’ mpya zaidi ya zile zilizotokea. Habari mbaya ni kwamba WHO wamesitisha huduma DRC kwa sababu gari la watumishi limechomwa moto kule.

“Ina maana itazidi, kwa hiyo tuendelee kuchukua hatua Mwanza, Kigoma, Rukwa Songwe na Dar es Salaam, ila kipekee nimpongeze Mganga Mkuu wa Mwanza amefanya kazi nzuri kama mgonjwa atatokea jinsi ya kumhudumia,” alisema.

Ummy alisema wameagiza mashine 70 za X-ray ambazo zitafungwa katika hospitali za rufaa za mikoa pamoja na mnashine 20 za X-ray za meno ambazo nazo zitafungwa katika hospital hizo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527