IRAN YASEMA IMEZIDISHA KIWANGO CHA MADINI YA URANI


Waziri wa Mambo ya Nchi za Kigeni wa Iran Mohammed Javad Zarif amesema  kuwa Iran imezidisha  ukomo wa viwango vya madini yake ya urani katika hifadhi zake, uliowekwa chini ya mkataba wa 2015 wa nyuklia. 


Shirika la habari la Iran - ISNA limeripoti kuwa Iran ilipitisha kiwango cha ukomo wa kilo 300 kwenye mpango wake. 

Marekani ilijiondoa kwenye mpango huo wa nyuklia mwaka jana na ikaiwekea Iran vikwazo vikali kama sehemu ya kampeni ya kuiongezea mbinyo mkali. 

Kwa kulipiza kisasi, mnamo Mei 8, Iran ikatangaza kuwa haitaheshimu tena viwango vya mwisho vilivyowekwa vya hifadhi zake za madini ya urani yaliyorutubishwa. 

Ilitishia pia kwenda mbali zaidi na kuachana na ahadi zake za nyuklia kama washirika waliobaki katika mkataba huo, ambao ni pamoja na Uingereza, China, Ufaransa, Ujerumani na Urusi, hawataisaidia nchi hiyo kutokana na vikwazo ilivyowekewa na hasa vya kuuza mafuta yake. 

Muda mfupi baada ya tangazo hilo la Iran kutolewa, Shirika la Umoja wa Mataifa la Kudhibiti matumizi ya nishati ya nyuklia - IAEA limethibitisha kuwa Iran ilipindukia ukomo wa viwango vyake vya madini ya urani.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527