RAIS MAGUFULI AAGIZA PORI LA SELOUS KUWA HIFADHI YA TAIFA IITWE ' NYERERE NATIONAL PARK'


Rais  Magufuli ameiagiza Wizara ya Maliasili na Utalii kukata eneo la ukanda wa juu wa pori la Selous na kulifanya kuwa Hifadhi ya Taifa na liitwe ‘Nyerere National Park’  ili kuenzi mawazo ya Hayati Baba wa Taifa.


Magufuli ametoa agizo hilo leo Ijumaa Julai 26, wakati akizindua ujenzi wa mradi wa kufua umeme wa Stieglers Gorge katika mto Rufiji mkoani ambapo amesema eneo litakalobaki waachiwe wawindaji waendelee na shughuli zao.

Amesema sababu ya kufanya hivyo ni kuongeza maeneo ya utalii hapa nchini ili kuendelea kukuza pato la taifa kutokana na fedha watakazolipa wataii.

“Kuna siri lazima niwaambie ndugu zangu,  kwenye pori la Selous kuna vituo vya uwindaji (hunting block) 47 vimeshachukuliwa, watu wanakuja na ndege hapa wanaua wanyama wanaondoka, bei yake ya chini kwa kituo ni Dola za Marekani 5, 000 ambazo ni sawa na Sh. milioni 10 za Tanzania kwa mwezi na ukilipa hiyo unaruhusiwa kuua hata nyati 10, kwa ujumla hii ‘Game Reserve’ haitupi faida.

“Kutokana na hali hii nataka  ‘Game Reserve’ ya Selous tuikate na iwe Hifadhi ya Taifa ili watalii wawe wanakuja hapa badala ya watu kuja kuwinda wanyama wetu, mataifa mengine hawafanyi sana hizi shughuli na uzuri Waziri wa Maliasili yuko hapa huu ndiyo ujumbe wako, kakae kwenye Wizara mkapunguze eneo la uwindaji, hilo limesemwa sana lakini utekelezaji umecheleshwa,” amesema Rais Magufuli.

Ameagiza pia fedha na dhahabu zilizorudishwa baada ya kuibiwa hapa nchini na kupatikana nchini Kenya zikatumike kujenga barabara ya lami kutoka lilipo pori la Selous hadi eneo la Fuga inakopita treni ya umeme ya Standard Gauge.

“Juzi nimepokea dhahabu zilizorudishwa kutoka Kenya nimepiga hesabu vizuri ni kama Sh bilioni nne au tano na fedha taslimu kama milioni 500, nataka hizo fedha zianze kutengeneza barabara ya lami kutoka hapa hadi eneo la Fuga ambazo ni kilometa 60 ili watu wakitoka Dar es Salaam kwa treni wakishuka pale Fuga wanatumia barabara hadi hapa kuja kutalii,” amesema.

Aidha ameagiza pia bwawa litakalojengwa kwa ajili ya mradi wa kuzalisha umeme lipewe jina la Mwalimu Nyerere kwani hayo yalikuwa mawazo yake na kufanya hivyo ni kumuenzi.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527