MAHAKAMA YAKWAMA KUTAZAMA MKANDA WA VIDEO KESI YA VIONGOZI 9 WA CHADEMA


 Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imekwama kuangalia video inayowahusu viongozi 9 wa CHADEMA akiwemo Mwenyekiti wa chama hicho Freeman Mbowe kutokana na upande wa utetezi kuipinga.

Pingamizi hilo liliwasilishwa na Wakili wa utetezi, Peter Kibatala baada ya Wakili wa Serikali Mkuu, Paul Kadushi kuiomba mahakama mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu,Thomas Simba kuandaa mazingira wezeshi ya kuonesha maudhui ya video iliyochukuliwa wakati wa kufunga kampeni za uchaguzi mdogo Jimbo la Kinondoni.

Upande wa mashitaka uliomba mahakama hiyo itumie Kituo cha Mafunzo cha Kisutu kuonesha maudhui hayo kwa sababu kina vifaa vinavyowezesha kuonekana kwa video hiyo vizuri.

Hata hivyo, Wakili Kibatala alidai upande wa mashitaka ulipaswa kuandika barua kwa uongozi wa mahakama kuomba kutumika kwa kituo cha mafunzo kuonesha maudhui hayo.

Pia amedai, walipaswa kuandaa vifaa vyote muhimu ikiwemo waya na projekta ambavyo vingewezesha kuonekana kwa video hiyo na sio wajibu wa mahakama kuandaa.

Kutokana na mvutano wa kisheria baina ya pande mbili, Hakimu Simba ameahirisha kesi hiyo hadi August 5, 6 na 7, 2019 kwa ajili ya kutoa uamuzi kama video itizamwe ama lah pamoja na kuisikiliza kesi hiyo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527