CYPRIAN MUSIBA APEWA SIKU 7 NA MAHAKAMA ZA KUWASILISHA UTETEZI WAKE DHIDI YA BENARD MEMBE


Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam imempa siku 7 mmiliki wa gazeti la Tanzanite, Cyprian Musiba na wachapishaji wa gazeti hilo kuwasilisha majibu dhidi ya madai ya Bernard Membe. 

Waziri huyo mstaafu wa Mambo ya Nje anataka kulipwa Sh 10 bilioni kwa kuchafuliwa na gazeti tajwa.


Uamuzi huo wa mahakama umetolewa jana Jumanne Julai 2, mbele ya Jaji Joaquine Demelo baada kupitia maombi ya wajibu maombi ya kutaka waongezewe muda wa kuwasilisha utetezi na majibu kinzani.

Jaji Demelo alisema wajibu maombi walitakiwa kuwasilisha utetezi na majibu kinzani ndani ya siku 21 baada ya shauri kufunguliwa Desemba mwaka jana lakini hawakufanya hivyo ambapo Musiba kupitia Wakili wake Majura Magafu waliomba kuongezewa muda japo wadai walipinga maombi hayo wakitaka yasikubaliwe.

“Mahakama imesikiliza hoja za pande zote mbili imeona kesi ina maslahi kwa umma hivyo ni bora na upande mwingine wakasikilizwa. 



"Hatuwezi kusikiliza shauri upande mmoja, kesi hii  ina maslahi kwa umma kuna haja ya kuusikiliza na upande wa pili, nawapa siku saba muwasilishe utetezi na hati ya kiapo kinzani,” alisema Jaji Demelo.

Jaji Demelo alisema upande wa waleta maombi kama watakuwa na hoja za kujibu utetezi wawasilishe kabla ya Agosti 8, mwaka huu ambapo shauri hilo la madai litaanza kusikilizwa Agosti 6, mwaka huu.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527