WAKAMATWA NA POLISI WAKIJIFANYA USALAMA WA TAIFA NA KUTAPELI WATU KAHAMA

Na Patrick Mabula - Kahama.

Jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga linawashikilia watu wawili Mrisho Zabron (37) na Mgema Patrick ( 25 ) kwa tuhuma ya kujifanya Maafisa Usalama wa taifa (TSI) na kuwatapeli watu pesa.

Kwa mujibu wa Kamanda wa polisi wa mkoa wa Shinyanga, ACP Richard Abwao amesema Zabron ambaye ni mkazi wa mtaa wa Nyasubi na Patrick mkazi wa Majengo walikamtwa juzi baada ya jeshi la polisi kuwawekea mtego na kufanikiwa kuwakamata.

"Siku ya tukio walijifanya maafisa usalama wa taifa walikwenda kwa mfanyabiashara Abdalah Moro wa mjini Kahama aliyekuwa amefungiwa godauni lake na TFDA na kujitambulisha maafisa usalama wa taifa walimwomba awapatie rushwa ya shilingi milioni tatu ili aweze kufunguliwa godauni lake lakini akatoa taarifa kwa jeshi la polisi",ameeleza.

Kamanda Abwao ameeleza kuwa baada ya jeshi la polisi baada ya kupewa taarifa hiyo na mfanyabiashara Moro juu watu hao waliokuwa wanajifanya maafisa usalama wa taifa lilikwenda kuweka mtego na kufanikiwa kuwakamata watuhumiwa wakiwa wanajiandaa kupokea kiasi cha fedha hizo walizokuwa wameomba.

Kamanda Abwao amesema jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi na utakapokamilika watafikishwa mahakamani na ametoa rai kwa watu kuwa makini na matapeli ambao wamekuwa wakitapeli wananchi kwa kutumia taasisi hiyo nyeti ya serikali.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post