TAKUKURU YAWASHA MOTO WALIOPIGA BILIONI 46 ZA LIBYA


Taasisi ya Kuzuia na kupambana na Rushwa (Takukuru), imetangaza kuwasaka watu wanne wanaodaiwa kutoweka na zaidi ya Sh bilioni 46, ambazo ni mkopo kutoka Serikali ya Libya ili kujenga Kiwanda cha Saruji mkoani Lindi.

Akizungumza katika mkutano na wanahabari jana, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Brigedia Jenerali John Mbungo, alisema fedha hizo kwa Serikali ya Tanzania na Serikali ya Libya, kama mkopo wenye riba.

Alisema kwa kuwa Serikali haifanyi biashara, fedha hizo zilikabidhiwa kwa kampuni ya MEIS Industries Ltd mwaka 2009 kwa ajili ya kujenga kiwanda hicho, lakini hadi sasa hakijawahi kuonekana na wahusika hawajulikani walipo.

“Mwaka 2009 Serikali hizi mbili zilitia saini mkataba ulioitaja kampuni ya MEIS Industrial Limited kama kampuni itakayopewa dola milioni ishirini za Marekani kwa ajili ya uwekezaji wa ujenzi wa kiwanda cha Saruji eneo la Machore mkoani Lindi.

“Fedha hizo zilitolewa kwa kampuni ya MEIS kama mkopo uliopaswa kurejeshwa kwa riba nafuu na kwa mujibu wa mkataba, mkopo huo ulipaswa kurejeshwa ndani ya miaka sita, yaani 2011 hadi 2017. Hata hivyo, hadi mwaka 2019 kampuni hiyo haijarejesha mkopo huo wala kiwanda cha saruji kilichokusudiwa kujengwa bado hakijajengwa,” alisema.

Alisema uchunguzi uliofanywa na Takukuru umebaini kuwa sehemu kubwa ya fedha hizo imetumika kwa matumizi mengine kinyume na makusudio ya Serikali jambo ambalo ni kosa.

Brigedia Jenerali Mbungo alisema wahusika wa kapuni ya MEIS ambao wanatafutwa ni Islam Ally Saleh Balhabou, Merey Ally Awadh Saleh, Sabri Ameir Kuleib na Abdallah Said Abdallah bin Aliya, ambao hadi sasa hawajulikani walipo.

Alisema zipo taarifa kuwa huenda wengine walikimbilia Visiwa vya Comoro na wengine nchini Uingereza, hivyo juhudi za kuwatafuta zinaendelea.

“Tunatoa wito kwa yeyote mwenye taarifa sahihi za mahali watuhumiwa hawa wanapoweza kupatikana wawasiliane nasi ili wakamatwe na kuja kujibu tuhuma hizi zinazowakabili kwa kuwa kosa hili liko chini ya kifungu cha 28(2) cha Sheria ya Kuzuia na kupambana na Rushwa namba 11 ya mwaka 2007,” alisema.

Akitoa ufafanuzi kuhusu mikopo iliyotolewa na Serikali ya Libya kwa Tanzania, alisema Serikali ya Libya katika miaka ya 1980 iliikopesha Serikali ya Tanzania mafuta ya petrol na dizeli kiasi cha tani 200,000 za ujazo ambayo kufikia mwaka 2005 ilikuwa ikiidai Serikali ya Tanzania Dola 201,000,000.

Alisema kutokana na fedha hizo, Serikali ya Libya ilisamehe nusu ya deni ambapo Seriali hizo mbili zilikubaliana namna ya kulipa dola 101,000,000 zilizobaki.

“Katika makubaliano haya, dola milioni 61 zilitakiwa kulipwa kwa mtindo wa madeni ya kitaifa, dola milioni 20 zilipwe kwa mpango maalumu na dola 20 milioni zifanye uwekezaji nchini Tanzania na baadaye zirudishwe Libya kwa riba nafuu,” alisema.

Alieleza katika mpango huo, kampuni hiyo ya MEIS ilipopewa fedha hizo kwa ajili ya kufanya uwekezaji nchini ambao ulitakiwa uwe umeshakamilika na urejeshaji wa fedha hizo nchini Libya kwa riba nafuu uwe umeshakamilika kufikia mwaka 2017.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527