SHEHENA YA MAGUNIA 455 YA MKAA YAKAMATWA KAHAMA IKISAFIRISHWA KWA LORI KUELEKEA JIJINI MWANZA

SALVATORY NTANDU

Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) kwa kushirikiana na Vyumbo vya Ulinzi wilayani Kahama mkoani Shinynga wamefanikiwa kukamata lori aina ya scania  lenye namba za Usajili T 656 AQC  likiwa limebeba shehena ya magunia ya mkaa 455 uliovunwa kwa njia isiyohalali.

Akizungumza na waandishi wa Habari Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya ya Kahama, ANAMRINGI MACHA amesema gari hilo limekamatwa na vyombo vya usalama baada ya kubaini kuwa mkaa huo ulikuwa hauna nyaraka zinazoonesha kuwa ulivunwa kwa uhalali.

Amesema serikali itaendelea kuchukua hatua kali za kisheria kwa watu watakaobainika kuvuna mazao ya misitu kiholela kwa manufaa yao binafsi jambo ambalo linasababisha uharibifu wa Mazingira.

MACHA amefafanua kuwa ni vyema watu wanaotaka kuvuna au kusafirisha mazao ya misitu wakafuata sheria na taratibu za uvunaji kwa kupata vibali kutoka ofisi za (TFS) ili kuepuka usumbufu unaoweza kujitokeza ikiwemo kutaifishiwa mali zao.

Kwa upande wake Meneja wa (TFS) Kahama JUMA ALLY amesema  Mmiliki wa lori hilo amejitokeza na kukubali kulipa faini ya zaidi ya shilingi milioni 24 ili aweze kupatiwa gari lake ambapo mpaka sasa anaendelea na taratibu za malipo.

Sanjari na hilo ALLY amesema kwa Mujibu wa sheria namba 14 ya mwaka 2012 kifungu namba 95 kinampa mamlaka ya kufanya tathimini ya mazao ya misitu ambayo yamekamatwa na kumlipisha faini mmiliki wa gari hilo.

Amefafanua kuwa   baada ya kukamilisha taratibu za malipo Mkaa huo gunia 455 zitataifishwa na serikali huku taratibu za kumkabidhi gari lake zitafuata.

Nae ELIAS NKEYE mmliki wa Lori hilo amesema atalipa faini hiyo ili kukomboa gari lake na kusema kuwa dereva na utigo wa gari hilo hawajulikani walipo na mmiliki wa magunia pia hakuweza kujulikana mara moja.

Nimeambatanisha na picha mbili

Mwisho.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527