WAZIRI UMMY ATOA RAI KWA VIONGOZI WA DINI PAMOJA NA WAZAZI KUSHIRIKIANA NA SERIKALI KUTOA ELIMU JUU YA MALEZI YA WATOTO


 Na.Faustine Gimu Galafoni,Dodoma.
Waziri wa Afya ,Maendeleo ya Jamii,jinsia Wazee na Watoto  Mhe.Ummy Mwalimu ametoa Rai kwa viongozi wa Dini,Taasisi pamoja na wazazi kushirikiana na Serikali  kutoa Elimu juu ya Malezi bora ya Watoto ili kupunguza vitendo vya kikatili dhidi ya watoto vinavyofanywa na watu wa karibu ikiwa ni pamoja na ulawiti. 


Mhe.Ummy ametoa Rai hiyo,Leo Mei 24,2019 bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la  Nyongeza la Mbunge wa Rombo Joseph Selasini aliyehoji kuwa watoto wananyanyaswa kwa kiasi kikubwa ikiwa ni pamoja na kulawitiwa ni lini serikali itatembelea mashuleni ili kuweza kutoa elimu dhidi ya unyanyasaji na kulawitiana kwa watoto. 


Katika majibu yake,Waziri Ummy amesema pamoja na majukumu ya kila siku kwa wazazi wanatakiwa kuwakagua mara kwa mara watoto wao huku akiomba viongozi wa dini kusaidia kuhubiri kwani sheria peke yake haiwezi kumaliza tatizo hilo. 


Aidha ,Waziri Ummy amesema serikali imekuwa ikifanya mikakati mbalimbali katika kudhibiti vitendo vya  Ukatili kwa wanawake na watoto kwa kutoa elimu ambapo pia kuna namba ya bure ambayo ni 116 husaidia kwa watu wanaofanyiwa vitendo hivyo kuwasiliana na mamlaka husika na kuna zaidi ya madawati  ya kijinsia 350   hapa nchini. 


Hata hivyo,Waziri Ummy amesema kuanzia Tarehe 16 Juni,2019 ambayo ni siku Muhimu ya Mtoto wa Afrika serikali itazindua ajenda ya kitaifa kuhusu wajibu wa Mzazi katika Malezi ya Mtoto.

 


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527