WANANCHI WASISITIZWA KUFUATA NA KUZINGATIA SHERIA ZA UHIFADHI


Naibu  Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe.Constantine Kanyasu amewataka wananchi wafuate sheria  kwa kujiepusha kuendesha shughuli za kibinadamu ndani ya Hifadhi ili kujenga mahusiano mazuri baina yao na Wahifadhi.

Pia, amewataka  wananchi kuwachukulia Wahifadhi hao   kama rafiki wa umma na watendaji waliotumwa na Serikali kulinda Maliasili  kwa niaba yao.

Akizungumza na  Watumishi  wa Pori la Akiba la Swagaswaga katika wilaya ya Chemba  jijini Dodoma,  Mhe. Kanyasu amesema Wahifadhi wamepewa jukumu la   kulinda hifadhi za Taifa na wamekuwa  wakifanya kazi nzuri ya kuifanya Tanzania iendelee kuwa na maeneo mazuri yaliyohifadhiwa.

''Sisi ni wa moja hakuna haja ya kujengeana uhasama kati  yetu,  Wananchi wafuate sheria za Uhifadhi  na Wahifadhi fuateni sheria wakati mnapokabaliana na Wananchi'' amesisitiza Kanyasu.

Amesema Wahifadhi wa Wanyamapori na Misitu wanazilinda rasilimali hizo kwa ajili wote, vitu kama mvua, hali ya hewa safi pamoja na mvua ni moja ya faida za moja kwa moja zinazopatikana kutokana na maeneo yaliyohifadhiwa vizuri.

Amesema Wahifadhi hao wameajiriwa kwa mujibu wa sheria hivyo hutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia maadili ya kazi zao na pale wanapokiuka sheria mamlaka zinazohusika huwachukulia hatua.

“Sisi kama Wizara tunaamini kwamba wahifadhi wetu wanafanya kazi nzuri, pale ambapo wamekuwa wakilaumiwa kwa kuwapiga na kuwanyanyasa watu kwa namna yoyote ile tumetuma Tume maalum kuchunguza na kuchukua hatua” Amesema

Mhe, Kanyasu amesema uchunguzi unapofanyika na ikathibitika kuwa tukio lililofanyika halikuongozwa na matumizi ya sheria na kuwepo kwa haki wizara imekua ikichukua hatua.

Ameeeleza kuwa Wahifadhi ni watu muhimu saba kwa vile bila wao hakuna uhifadhi unaoweza kuendelea nchini akibainisha kuwa baadhi ya watu wamekuwa wakipinga juhudi za uhifadhi kwa kuwatetea watu wanaovunja sheria.

Kuna watu wanatamani kuona  misitu na wanyamapori wote tunawamaliza ili wapate maeneo ya malisho na kilimo, Nawambieni tukithubutu kufanya hivyo huu ndo utakuwa mwisho wetu wa maisha" Amesisitiza Mhe.Kanyasu

Amesema yapo madhara makubwa yanayoweza kutokea kama hakutakuwa na uhifadhi imara ikiwemo maeneo mengi ya nchi kugeuka kuwa jangwa kutokana na uharibifu wa misitu, ukosefu wa mvua, ukosefu wa maji, chakula na ukosefu wa hewa safi.

Kwa upande wake, Meneja wa Pori la Akiba la Swagaswaga, Alex Choya  amesema kuwa kumekuwa na tuhuma za vitendo vya ukatili dhidi ya raia vinavyofanywa na baadhi ya askari wa hifadhi za Taifa na kutoa wito kwa wananchi wote wenye ushahidi na taarifa juu ya vitendo hivyo kuziwasilisha ili hatua stahiki zichukuliwe.

Amesisitiza kuwa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) hairuhusu askari kufanya vitendo vya ukatili na unyanyasaji dhidi ya raia badala yake imekua ikiwahamasisha wananchi kushiriki kikamilifu katika ulinzi wa rasilimali zinazowazunguka.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post