WAKURUGENZI WA HALMASHAURI 10 WATAKIWA KUHAKIKISHA MRADI WA TIMIZA NDOTO YAKO UNATEKELEZWA KIKAMILIFU

Na Mwandishi Wetu
Wakurugenzi 10 wa Halmashauri za Wilaya wametakiwa Kuhakikisha kuwa mradi wa timiza ndoto zako kwa wasichana Balehe waliopo mashuleni na walio nje ya mfumo wa elimu unatekelezwa kama ilivyopangwa na Serikali ili kuleta matokeo chanya.

 
Akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama Mei 25, 2019 Wilayani Bahi mkoani Dodoma wakati wa uzinduzi wa mradi huo, Katibu Mkuu Ofisi hiyo anayeshughulikia Sera Uratibu na Uwekezaji Bi. Dorothy Mwaluko amesema kuwa dhamira ya Serikali ni kuona mradi huo unaleta ukombozi wa kweli kwa mtoto wa kike.

“ Waliopo shuleni na nje ya mfumo wa elimu ni vyema mkatambua kuwa mradi huu ni fursa yakuwawezesha kujikwamua kiuchumi na kuepeuka vishawishi na maambukizi ya Virusi vya ukimwi kwani Serikali inatambua kuwa kumuwezesha mtoto wa kike ni kuiwezesha jamii nzima”Alisema Bi. Doorthy.

Mradi huu unatekelezwa katika mikoa ya Dodoma, Morogoro na Singida ambapo jumla ya Halmashuri 10 katika mikoa hiyo zinanufaika.Utekelezaji wake unatokana na usaidizi wa fedha kutoka kutoka Mfuko wa Dunia kwa ajili ya kuendeleza
mapambano dhidi ya maambukizi ya Virusi vya UKIMWI na athari zake.

Akifafanua amesema kuwa watekelezaji wa mradi huo wanalo jukumu la kuwajengea uwezo wanaufaika ili hata baada ya kipindi cha mradi waweze kujitegemea na kuondokana na utegemezi kutoka kwa serikali ambapo kwa sasa wanafunzi kutoka Kaya masikini wanawezeshwa kupata taulo za kujisitiri pamoja na mahitaji mengine ikiwemo sare za shule.

Aliongeza kuwa wanafunzi wote wanapaswa kutambua kuwa
Serikali inawekeza fedha nyingi katika mradi huo kwa kutambua umuhimu wa kundi hilo ili kujikwamua kielimu na kutumia vyema vipaji walivyo navyo.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Bahi Mhe. Mwanamisi
Mukunda akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa huo Dkt. Binilith Mahenge amasema kuwa mradi huo umesaidia kuongeza kiwango cha ufaulu katika Wilaya hiyo, mahudhurio ya wanafunzi shuleni yameongezeka kwa kiwango kikubwa.

“Tunaishukuru Serikali ya Awamu ya Tano kwa kutuletea mradi huu katika Wilaya yetu kwani umeonesha mafanikio makubwa kwa kipindi cha majaribio ambacho umetekelezwa kwani umewanufaisha Wanawake Vijana wenye umri wa kati ya miaka 10- 24”, alisisitiza Mhe. Mwanahamisi.

Akifafanua amesema kuwa mradi huo umefikia Kaya 265 na
wasichana 129 unawanufaisha wasichana balehe waliopo shuleni na wale wa nje ya shule 45.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS) Dkt. Leonard Maboko amesema kuwa mradi huo ni wa miaka 3 na unatekelezwa katika mikoa 3 ambapo wanufaika wa mradi walio nje ya shule watajengwewa uwezo kwa kupewa stadi za maisha.

Alitaja sababu za kuwalenga wasichana wanaobalehe Dkt. Maboko amesema kuwa ni pamoja na kundi hilo hilo kuwa waathirika wakubwa ambapo asilimia 80 ya maambukizi ya VVU yamewaathiri vijana wa kundi hilo.

Mmoja wa wazazi wa wanafunzi walionufaika na mradi huo Bi Mayasa Mussa amesema kuwa wanafunzi wanafurahia mradi huo na ari ya kwenda shule imeongezeka kwani kila mwezi wanapokea elfu 25,000/- kwa mwezi kuwawezesha kukidhi mahitaji muhimu ya wanafunzi hao ikiwemo kupata taulo za kike, sare za shule na mahitaji mengine.

Mradi wa Timiza ndoto zako unatekelezwa katika mikoa 3 na
Halmashuri na Halmashuri 10 ukilenga kuwawezesha wasichana waliobalehe wakiwa mashuleni na wale walio nje ya mfumo wa elimu.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527