JWTZ WATUMIA NDEGE YA ATCL KUSAFIRISHA WAPIGANAJI KUISHIRIKI ULINZI WA AMANI DARFUR


Na Luteni Selemani Semunyu
Maafisa na Askari wa jeshi la Ulinzi la wananchi wa Tanzania (JWTZ), wanaoshiriki Ulinzi wa Amani katika  Jimbo la Darfur nchini Sudan kwa Mara ya kwanza  kwa kipindi cha Miaka 10 ya Ulinzi wa Amani Jimboni humo wametumia Ndege ya Shirika la Ndege ya  Serikali ya ATCL ikiwa ni kuunga mkono jitihada za Mhe Rais wa  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu katika  kulifanya Shirika hilo linapiga hatua zaidi kwa maslahi ya Shirika na Taifa kwa ujumla.


Akizungumza na Waandishi wa Habari Mkuu wa Mafunzo na Utendaji Kivita wa JWTZ Meja Jenerali Alfred Kapinga amesema Jeshi ni Taasisi inayoongozwa na Uzalendo,uadilifu, uhodari  hivyo ni faraja kubwa kwa Jeshi  na wapiganaji kuunga mkono jitihada za Serikali katika Kuboresha Uchumi  ikiwa ni  sehemu ya mchango wao katika kuonesha  uzalendo kwa vitendo kwa  kutumia vitu vya nyumbani kwa maslahi mapana ya Taifa.

“ Tumekuwa tukitumia Ndege zetu za Jeshi lakini tumekuwa tukitumia Ndege za mataifa mengine kwa Mikataba kutoka Umoja wa Mataifa lakini sasa ni faraja kwani tumefanikiwa kuwashawishi Umoja wa Mataifa kutumia Ndege zetu” Alisema Meja Jenerali Kapinga.

Aidha,Meja Jenerali kapinga alisema   mbali na kutumia Ndege hiyo lakini aliwaasa Maafisa na Askari hao kuhakikisha wanapeperusha vema Bendera ya Nchi na kuendelea kuitangaza kwa  sifa nzuri za Utendaji Kimataifa.

Kwa Upande wake Mkurugenzi wa Shirika la Ndege la la Tanzania (ATCL),  Mhandisi Ladislaus Matindi  Alisema ni Fursa Nzuri kwa ATCL na wanalishukuru Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania kupitia kwa mkuu wa majeshi ya Ulinzi  kwa Mchango mkubwa   kufanikisha kupata tenda hiyo.

“ Namshukuru Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi  Jenerali Venance Mabeyo na watendaji wake kwa Uzalendo wake na kuhakikisha anafanikisha ATCL kupata fursa kwa mara ya kwanza na hii itakuwa mwanzo mzuri na tutahakikisha tunaitumia vizuri  fursa hii kujitangaza zaidi Kimataifa kwa maslahi  ya Nchi “ Alisema Mhandisi Matindi.

Vilevile  Mhandisi Matindi aliongeza kuwa Ndege ya Dream Liner ina uwezo wa kusafiri kwa saa 12 bila kusimama, hivyo kwa  kutumia saa tatu kusafiri kutoka hapa mpaka nchini Sudan  ni sehemu ndogo ya Uwezo wake na ni nafasi ya kuwajaribisha watendaji wa Ndege wa ATCL katika kuhudumia safari Ndefu.

Naye Kamanda wa Kikosi cha TANZBATT- 13,  Luteni Kanali Khalfan Kayage  anayekwenda na  Kikosi hicho  alisema kuwa  inawapa nguvu kupeperusha Bendera yetu kupitia Ndege na ameahidi kufanya kazi kwa Bidii kuendeleza jina na sifa nzuri ya Tanzania Kimataifa.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527