WALIMU 86,000 WAIDAI MABILIONI SERIKALI

Na.Faustine Gimu Galafoni,Dodoma.

Imeelezwa kuwa kuna jumla ya walimu zaidi ya  86,000 wanaidai Serikali kwa madeni ya Malimbikizo mbalimbali ikiwa ni pamoja na Malimbikizo ya Mishahara na fedha za likizo .


Hayo yamesemwa jana  April 15 bungeni jijini Dodoma na Naibu waziri wa nchi ,ofisi ya Rais na Serikali za mitaa ,TAMISEMI Mwita Waitara wakati akijibu swali la Mbunge la Mbunge wa viti Maalum Kiza Husein aliyetaka kujua  namna ya ulipaji fedha za likizo kwa walimu.


Katika majibu yake  Naibu Waziri wa  TAMISEMI, Mwita Waitara alisema Serikali ina nia nzuri kuhakikisha inalipa walimu kwa wakati na kwamba wapo walimu 86,000 ambao wanaidai Serikali zaidi ya Shilingi Bilioni  43 .

Awali, katika swali lake la msingi mbunge huyo alisema Serikali imekuwa ikiwapandisha madaraja walimu lakini haitoi malipo stahiki kwa madaraja hayo mapya kwa kipindi kirefu tangu walipopanda madaraja yao.


Akijibu swali hilo, Waitara alifafanua kuwa Serikali ilisitisha kupandisha walimu na watumishi wengine madaraja katika mwaka wa fedha 2015/16 na 2016/17 kutokaana na uhakiki wa watumishi.


Waitara alisema kutokana na sababu hiyo ni kweli wapo watumishi ambao walipandishwa madaraja hawajalipwa mishahara mipya, wapo waliopata mishahara mipya na baadaye kuendolewa na wengine hawakupandishwa licha ya kuwa na sifa.

Alisema ili kurekebisha changamoto hizo, Serikali ilitoa maelekezo kuanzia Novemba 2017 kwa waajiri wote wakiwamo wakurugenzi wa mamlaka za serikali za mitaa kuhuisha barua za kuwapandisha madaraja watumishi hao ili waweze kulipwa stahili zao .

Kwa upande wake Naibu waziri wa Ofisi ya Rais,Utumishi na Utawala Bora Mhe.Mary Mwanjelwa ametoa ufafanuzi  juu ya suala la  muda wa kukaimu kwa watumishi wa umma ambapo ukomo wake ni   miezi sita zaidi ya hapo    mwajiri anatakiwa kuandika barua tena ya ombi la kuendelea kukaimu na sababu zake.

Hii imekuja baada ya  mazoea kwa baadhi ya wakurungezi hapa nchini kuendelea kuwakaimisha  watumishi wao wakiwemo maafisa watendaji wa vijiji na kata kwa muda mrefu.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527