VYAMA VYA USHIRIKA VYASHAURIWA KUKOPA FEDHA KWENYE MABENKI KWA AJILI YA WANACHAMA WAO

Bashiri Salum,Wizara ya Kilimo Arusha
Vyama vya Ushirika vimeshauriwa kukopa fedha kwenye Mabenki kwa ajili ya  wanachama wao kwa kuwa waliowengi hawakopesheki hivyo kufanya shughuli za kilimo kuwa ngumu.


Akizungumza katika kikao kilicho wakutanisha Maafisa Ushirika, umwagiliaji na afisa kilimo  Mkoani Arusha Naibu Waziri Kilimo Mhe. Omari Mgumba amesema miundombinu mingi ya umwagiliaji inahitaji marekebisho makubwa  ili kuweza kutumiwa na wakulima.

Aidha miundombinu hiyo imekosa ukarabati kutokana na wakulima kutokuwa na mitaji ya kutosha na kutoaminiwa na taasisi za fedha kusaidia ukarabati huo.

Ameshauri tume ya Ushirika kuvisimia vyama vya ushirika ili viweze kukopa fedha Benki Kwa ajili ya wanachama lengo likiwa ni kufanya ukarabati Wa miundombinu ya umwagiliaji ambapo kila mwanachama atawajibika kuchangia huduma hiyo.

Hatuwezi kufanya Kilimo cha kibiashara Kwa kutegemea mvua ambazo Nazo zimekuwa haziyabiriki nawashauri tume ya Ushirika na tume umwagiliaji kusimamia vyama hivyo kwenye skimu mbalimbali za umwagiliaji kukopa fedha ambazo zitatumika kurekebisha miundombinu ya umwagiliaji badala ya kutegemea serikali .alisema Mhe. Naibu Waziri

Naibu Waziri aliwataka maafisa ugani kuwafikia wakulima na kuelimisha namna ya kutumia na kutoa elimu juu ya matumizi bora ya viuatilifu vya mimea ili kupambana na visumbufu vya mazao ambavyo vimekuwa vikimsababishia mkulima hasara kubwa.

Naye afisa Umwagiliaji wa kanda mhandisi Juma Mdete amesema katika ukanda huo eneo ambalo linafaa kwa kilimo cha umwagiliaji ni hekta elfu 40 kati ya hilo linalotumika ni  hekta elifu 24 tu

Amesisitiza kwamba pamoja na matumizi kidogo ya eneo la umwagiliaji lakini maeneo yanayomwagiliwa yanasaidia upatikanaji wa chakula wakati wa ukame.

Akichangia wakati wa mjadala huo Afisa Kilimo Mkoa wa Arusha Bwana Daniel Loiruck amethibitisha kwamba ukiondoa Magonjwa ya mlipuko na uvamizi wa visumbufu vya mimea  maafisa kilimo wamekuwa wakijitahidi kuwafikia wakulima ili kutatua changamoto zinazowakabili.

Naye mwenyekiti wa chama cha mapinduzi mkoani Arusha bwana Loata Erasto Sanare  akamueleza Mhe. Naibu waziri kwamba hali ya ukame mkoani humo ni kubwa hivyo kuishauri serikali kuanza kufikiri njia mbadala ya kupambana na hali hiyo.

‘Msimu wa kilimo upo katikati lakini mpaka sasa hakuna mvua na tumezunguka sehemu mbalimbali hapa arusha mahindi yamekauka hata mvua ikinyesha  haiwezi kuleta mabadiliko tunaishauri serikali kufikiri mbinu za kukabiliana na hali hiyo’. Alisisitiza bwana Loata  Sanare


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527