PROF. PALAMAGAMBA KABUDI: SHERIA YA NDOA YA 1971 NI YA KIMAPINDUZI

WAZIRI wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi amesema Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 ni Sheria ya kimapinduzi ambayo ilikuja nchini kwa wakati muafaka na kufafanua kuwa anaionasheria hiyo kuwa ni ya kimapinduzi kwa kuwa nchi nyingi duniani zimeshindwa kuwa na Sheria kama hiyo.


Prof. Kabudi alisema hayo bungeni juzi wakati alipokuwa akichangia hoja ya Bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria iliyowasilishwa Bungeni na Waziri wake Dkt. Augustine Mahiga.

Prof. Kabudi alisema suala hilo baada ya wabunge waliokuwa wakichangia hoja ya Dkt. Mahiga kutaka Sheria hiyo ya Ndoa ifanyiwe marekebisho hasa katika kipengele cha umri wa mtoto wa kike kuolewa.

Aliwataka Wabunge waache kuchukulia kipengele cha umri wa mtoto wa kike kuolewa kama kigezo cha kuifanya sheria hiyo kuwa mbaya na kwamba yapo mambo maengi mazuri ndani ya sheria hiyo kama vile kumuwezesha mwanamke aliyeolewa kumiliki mali huku akitumia jina la baba yake kwani enzi za ukoloni jambo hilo halikuwezekanika.

Alisema kuwa umri wa mtoto wa kike kuolewa ni jambo nyeti sana na litasababisha ugomvi hata miongoni mwa wabunge kwani hata nchi zilizoendelea akiitolea mfano Uingereza umri wa mtoto wa kike kuolewa ni miaka 16 na kuongeza kuwa wasichana hawaolewi kwa sababu ya fursa mbalimbali za elimu na mwamko.

Prof. Kabudi aliwataka wabunge kuisoma vizuri sheria kwani ina mambo mengi mazuri ambayo imeyaweka na makubwa hivyo ni vizuri wakaielewa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post