SHAUKU YA MAPINDUZI YA KIJESHI YATANDA SUDAN

Jeshi la Sudan limetangaza kuwa litatoa taarifa muhimu hivi karibuni, hali inayohisiwa kuwa utawala wa Rais Omar al-Bashir huenda ukafikia kikomo hivi karibuni.

Wanajeshi wametanda katika makazi rasmi ya rais mapema asubuhi ya leo, shirika la Habari la kimataifa la AFP linaripoti.

Jeshi pia limezingira njia zote muhimu za kuingia na kutoka mji mkuu wa Khartoum.

Magari yaliyosheheni wanajeshi wenye silaha yameegeshwa kwenye barabara zote muhimu na madaraja kwenye mji mkuu, shirika la habari la Reuters linanukuu mashuhuda.

Matangazo ya kawaida ya redio ya serikali yamekatishwa na kwa sasa zinapigwa nyimbo za ukombozi.

Raia wanaimba jwa furaha, "serikali imeangushwa. Tumeshinda," shirika la Reauters linaripoti.

Maelfu ya watu wamo barabarani wakijaribu kuelekea makao makuu ya wizara ya ulinzi kuungana na waandamanaji ambao wamekuwa wakishinikiza rais Bashir kubwaga manyanga baada ya miaka 30 madarakani.
Picha hii inaashiria nafasi ya wanawake katika maandamano dhidi ya serikali ya Sudan.

Mwanahabari mmoja maarufu na anayeheshimika nchini Sudan, Yousra Elbagir ameandika kupitia mtandao wake wa kijamii wa twitter kuwa baadhi ya viongozi waandamizi wa serikali wanakamatwa na wanajeshi, na kuwa uwanja wa ndege jijini Khartoum umefungwa.

Hii leo, kulipangwa kufanyika maandamano ya wafuasi wa Bashir ambao walitaka kuonesha uungaji mkono wao kwa kiongozi huyo lakini kuna ripoti kuwa maandamano hayo yamekatazwa.

Maandamano dhidi ya Bashir yalianza toka mwezi Disemba. Awali maandano yalianza kwa kupinga kupanda kwa bei ya vyakula lakini yamekuwa makubwa na kubadili lengo na kutaka kumng'oa rais madarakani.
Historia ya Rais Omar al-Bashir kwa ufupi:Rais Omar Bashir 'amekalia kuti kavu'
  • Apambana katika jeshi la Misri kwenye vita dhidi ya Israeli mwaka 1973
  • Achukua hatamu ya madaraka Sudan baada ya mapinduzi ya kijeshi mwaka 1989
  • Ampatia hifadhi kiongozi wa al-Qaeda Osama bin Laden katika miaka ya 90.
  • Awa kiongozi wa kwanza wa nchi kufunguliwa mashtaka ICC mwaka 2009.
  • Aingia makubaliano ya amani na waasi wa Sudan Kusini 2005.
  • Akubali Sudan Kusini ijitenge 2011, na kupoteza robo tatu ya utajiri wa mafuta.
  • Hana mtoto, na maisha yake binafsi ni ya usiri mkubwa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527