BABA MZAZI AFIKISHWA MAHAKAMANI KWA KUOA NA KUZAA NA MTOTO WAKE

Mkazi wa kijiji cha Mwanzamiso wilayani Misungwi mkoa wa Mwanza, Jacob Shabani (30) amefikishwa katika Mahakama ya wilaya hiyo kwa tuhuma ya kumuweka kinyumba mwanaye na kuzaa naye watoto wawili.

Akisoma hati ya mashataka mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Misungwi, Erick Marley juzi, mwendesha mashitaka wa polisi, Ramsoney Salehe alidai mshtakiwa alimuweka kinyumba mwanaye wa kumzaa kuanzia mwaka 2015 hadi mwaka jana.

Alidai kuwa mshitakiwa alimuweka kinyumba mwanaye huyo mwenye umri wa miaka 17 na kumzalisha watoto wawili na kwamba alikuwa akiishi nae chumba kimoja.

Mwendesha mashtaka huyo aliendelea kudai kuwa, kwa sasa amebaki mtoto mmoja mwenye umri wa mwaka mmoja na mwingine aliyekuwa na umri wa miaka mitatu alifariki dunia.

“Mtuhumiwa alibainika anaishi na mwanaye wa kike chumba kimoja na kulala nae kitanda kimoja na alikamatwa baada ya wananchi kutoa taarifa kuhusu tukio hilo,” alidai Salehe. Hata hivyo, mshtakiwa huyo alikana makosa hayo.

Upande wa mashtaka ulieleza kuwa upelelezi umekamilika.

Hakimu Marley aliahirisha shauri hilo hadi Aprili 23 kesi hiyo itakapoanza kusikilizwa na mtuhumiwa alirudishwa rumande baada ya kukosa mdhamini.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527