JENERALI MABEYO AWAONYA WANAOTOA KAULI ZA UCHOCHEZI


Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Jenerali Venance Mabeyo, amesema hivi sasa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) linafuatilia kwa karibu kauli za uchochochezi zinazotolewa na baadhi ya watu nchini.

Jenerali Mabeyo ametoa kauli hiyo mjini hapa leo Jumamosi Aprili 13, wakati akizungumza kwenye uzinduzi wa mji wa Serikali katika eneo la Mtumba mjini Dodoma mbele ya Rais Dk. John Magufuli.

Ingawa hakutaja kauli hizo za uchochezi zinatolewa na akina nani, Jenerali Mabeyo alisema JWTZ liko tayari kukabiliana na tishio lolote la amani nchini.

“Pamoja na hayo, hali ya usalama wa nchi iko tulivu kwa kuwa Tanzania haina mgogoro na nchi jirani na uwepo wa migogoro katika nchi zinazopakana na Tanzania, JWTZ tuko tayari kukabiliana na tishio lolote la amani litakalosababishwa na migogoro katika nchi jirani,” amesema.


Kuhusu ujenzi wa nyumba na ofisi za Serikali, Jenerali Mabeyo amesema kwa kiasi kikubwa kazi hiyo imefanywa na vijana wa JKT na imefanyika kwa miezi mitano.

Amesema kwa kuwatumia vijana hao, Serikali imeokoa takribani Sh2.1 bilioni,  huku akieleza kazi yote hiyo imefanyika kwa Sh5 bilioni.

“Mheshimiwa Rais vijana hawa wamefanya kazi kubwa sana, naomba kwa ridhaa yako utoe neno lolote la kuwafariji ila kwa upande wa maofisa nitaomba ruksa yako niwafanyie kitu na askari ambao wameajiriwa hao nitajua cha kuwafanyia,” amesema.



Wakati huo huo, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk. Binirith Mahenge aliwakaribisha wananchi wakawekeze mkoani Dodoma kwa kuwa kuna mazingira mazuri ya uwekezaji.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527