Waziri Mpango Ateta Na Wafanyakazi Na Kuhimiza Maadili Na Uwajibikaji Kazini

Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Isdor Mpango amekutana na Watumishi wa Wizara hiyo na kuzungumza nao namna bora ya utekelezaji wa  majukumu ya Wizara ili kusukuma kasi ya maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Akizungumza katika kikao hicho Dkt. Mpango alisema Wizara ya  Fedha na Mipango ni kitovu cha Serikali hivyo  Watumishi wote wa Wizara wanawajibu wa kutekeleza majukumu kwa kuzingatia nidhamu, maadili, sheria, kanuni na  taratibu za utumishi wa Umma ili kuongeza tija.

Amesema kila mtumishi anawajibu wa kufanya kazi kwa weledi, bidii na kushirikiana na kila mmoja katika nafasi yake ili kuboresha utendaji kazi na kukuza uhusiano mahala pa kazi.

Aidha Waziri Mpango aliwapongeza Watumishi wa Wizara hiyo kwa kazi wanazozifanya hususan kazi ya uandaaji wa Bajeti Kuu ya Serikali, Uchambuzi wa Sera za Taifa na uanzishwaji wa mfumo mpya wa ukusanyaji wa mapato ya Serikali kwa njia ya Kielektroniki-GePG.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Khatibu Kazungu amemhakikishia Waziri Mpango kuwa watatekeleza maelekezo yote aliyoyatoa kwa ukamilifu ili kuboresha utendaji kazi wa Wizara hiyo.

Mwisho.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
Wizara ya Fedha na Mipango


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527