WATUHUMIWA WA MAUAJI YA WATOTO NJOMBE WAPANDISHWA MAHAKAMANI

Washukiwa watatu wa utekaji na mauaji ya watoto wa chini ya miaka 10 wilayani Njombe, wamepandishwa mahakamani hii leo.

Watuhumiwa hao waliowekwa wazi kwa mara ya kwanza hii leo ni Nasson Kaduma, Joel Nziku na Alphonce Danda.

Wote wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe.

Nje ya mahakama hiyo ulinzi mkali wa polisi umeimarishwa na msafara wa watuhumiwa hao ukisindikizwa na magari sita ya polisi.

Watoto takribani 10 wameshauawa toka visa hivyo vya kutamausha kuanza kuripotiwa mwezi Disemba.

Miili ya watoto hao imekutwa ikiwa imenyofolewa baadhi ya viungo kama matumbo, vidole, pua na macho, wauaji hao pia wamekuwa wakinyofoa viungo vya siri vya watoto hao.

Mamlaka nchini Tanzania zimekuwa zikihusisha mauaji hayo na imani za kishirikina, waganga wa kienyeji wanalaumiwa kwa kuwaaminisha watu kuwa viungo vya binaadamu vinavuta bahati na utajiri.

Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa Ijumaa aliliambia Bunge kuwa tayari watu 29 wameshakamatwa kutokana na matukio hayo, na kusema kuwa uchunguzi bado unaendelea.

Miongoni mwa waliokamatwa ni wafanyabiashara maarufu wa eneo hilo pamoja na waganga wa jadi.

Chanzo:Bbc

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527