MAHAKAMA YAANZA KUSIKILIZA KESI YA MWALIMU ALIYEUA MWANAFUNZI

 
Picha hii haihusiani na habari

Mahakama kuu kanda ya Bukoba, leo imeanza kusikiliza kesi ya mauaji ya kukusudia inayomkabili Herieth Jerald ambaye ni mwalimu wa shule ya msingi Kibeta iliyoko Manispaa ya Bukoba.

Mwalimu huyo pamoja na mwenzake, Respicius Patrick wanadaiwa kutekeleza mauaji ya mwanafunzi wa darasa la tano katika shule hiyo aliyejulikana kwa Sperius Eradius aliyekuwa na umri wa miaka 14, akimtuhumu kuiba pochi yake.

Mwanafunzi huyo Sperius Eradius katika kesi hiyo anadaiwa kuuawa na walimu hao kwa kupigwa Agosti 27 mwaka jana, akidaiwa kuiba pochi ya mwalimu Heriet Jerald baada ya kumpokea mizigo wakati akiingia kazini.

Mahakama imeelezwa na mwendesha mashtaka kiongozi wa serikali, Chema Maswi kuwa washtakiwa hao walimuua kwa kukusudia mwanafunzi huyo katika eneo la shule ya msingi Kibeta, ambapo washtakiwa walikana mashtaka hayo.

Mshtakiwa mmoja kati ya sita waliokuwa wameletwa mahakamani hapo Benidius Benezeth ambaye ni mwendesha pikipiki aliyemsafirisha mwalimu Herieth Jerald alitoa ushahidi dhidi ya mwalimu huyo na kudai kuwa wakati akimsafirisha hakuona kama katika kikapu alichokuwa amebeba kuna pochi maana hakukikagua.

Baada ya kesi hiyo kuhairishwa hadi Februari 08 mwaka huu ushahidi utakapoendelea kutolewa, mwendesha mashtaka kiongozi wa serikali Chema Maswi ameeleza mwenendo wa kesi hiyo kwa upande wa serikali.
Chanzo- EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527