MBOWE ATUMA SALAMU ZA POLE KWA SUMAYE,AMTAKIA UPONAJI WA HARAKA

Mwenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Freeman Mbowe licha ya kuwa gerezani amemtumia salamu za pole Waziri Mkuu Mstaafu Fredrick Sumaye ambaye alipatwa maradhi ya ghafla alipokuwa mkoani Tanga.

Taarifa ya salamu hizo zimetolewa na chama chake ambapo amesema, "Mwenyekiti Freeman Mbowe ambaye bado yuko mahabusu Gereza la Segerea na Mbunge Esther Matiko, wamemtumia salaam za pole na kumtakia uponaji wa haraka Sumaye ili arejee katika siha njema"

Aidha taarifa ya chama hicho imeeleza kuwa Sumaye anaendelea vizuri na matibabu chini ya uangalizi wa madaktari wa Jakaya Kikwete Cardiac Institute (JKCI) alikohamishiwa baada ya kupokelewa Hospitali ya Taifa Muhimbili akitokea Hospitali ya Mkoa wa Tanga.

Aidha Katibu Mkuu wa Chama, Dkt. Vincent Mashinji, Mjumbe wa Kamati Kuu na Waziri Mkuu Mstaafu Edward Lowassa, Mwenyekiti wa Baraza la Vijana wa CHADEMA Patrick Ole Sosopi pamoja na viongozi wengine wa Chama ngazi na maeneo mbalimbali ya nchi, wamefika hospitalini hapo kumjulia hali.


Mzee Sumaye alipatwa na shida ya afya mapema juzi akiwa mkoani Tanga ambako alikuwa anaendelea na ratiba ya shughuli mbalimbali za Chama mkoani humo.


Kabla ya kuwasilishwa Muhimbili Sumaye alilazwa Hospitali ya Bombo kabla ya kuletwa Dar es Salaam kwa ajili ya uchunguzi zaidi wa afya yake.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527