MTOTO MWINGINE AUAWA NJOMBE


Mtoto wa miaka 10, ambaye ni mwanafunzi wa darasa la pili, amekutwa ameuawa kikatili na mwili wake kutelekezwa kichakani eneo la Lupembe, wilayani Njombe.

 Kamanda wa Polisi mkoa wa Njombe Renata Mzinga, amesema kuwa maiti hiyo iliokotwa karibu na nyumbani kwao na mtoto huyo, baada ya majirani kuanza kumtafuta mara tu baada ya kupata taarifa kutoka kwa wazazi wake kuwa mtoto wao haonekani.

“Mtoto alipotea tangu saa 12, lakini wazazi wake walianza kumtafuta majira ya saa nne ndo wakakuta ametupwa karibu tu na nyumbani kwao, baada ya mtoto kwenda kucheza kwa jirani ilipofika saa moja hajarudi, walienda kutoa taarifa kwa majirani na polisi, sasa wakaanza kutafuta mpaka wakakuta hiyo maiti, haikupita siku nzima, ni masaa machache sana”, amesema Kamanda Mzinga.

Matukio hayo ya watoto kuuawa yamekuwa yakitokea mara kwa mara mkoani Njombe na taarifa zake kufikishwa Bungeni, jambo ambalo Waziri wa Mambo ya Ndani Kangi Lugola amesema kwamba jeshi la Polisi linafanyia kazi kuweza kuwabaini wauaji.
Chanzo-EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527