WATOA HUDUMA ZA VVU NA UKIMWI WAHAMASISHWA KUONGEZA NGUVU KUTAFUTA WALIOACHA KUTUMIA DAWA ZA ARVs



Watoa Huduma za VVU na UKIMWI mkoani Shinyanga wametakiwa kuongeza juhudi za kuwatafuta,kuwarudisha na kuhakikisha Watu wanaoishi na Maambukizi ya Virusi vya UKIMWI waliopotea katika huduma wanaendelea kutumia dawa za kupunguza makali ya VVU.


Wito huo umetolewa Februari 20,2019 na Mratibu wa Kudhibiti na Kupambana na Ukimwi mkoa wa Shinyanga, Dkt. Peter Mlacha wakati akifunga warsha ya Watoa Huduma za VVU na UKIMWI mkoani Shinyanga.

Warsha hiyo iliyodumu kwa muda wa siku tatu iliyoandaliwa na Asasi ya kitaifa inayolenga kutokomeza UKIMWI kwa watoto na familia, Ariel Glaser Pediatric AIDS Healthcare Initiative (AGPAHI) ilijikita zaidi katika kujadili na kupanga mikakati namna ya kukabiliana na changamoto ya wateja kupotea katika huduma. 

Dkt. Mlacha alisema ili kuondokana na changamoto ya wateja kupotea katika huduma,watoa huduma za VVU na UKIMWI wanayo nafasi kubwa ya kuwarudisha kwenye huduma wateja hao.

“Ili Mteja azingatie dawa zake vizuri ni lazima awe na elimu ya kutosha kuhusu dawa,VVU na UKIMWI kwa ujumla, hakikisheni mnawapa elimu kwani takwimu zinaonesha kuwa wateja wengi wamekuwa wakipotea katika huduma kwenye hatua za mwanzo kabisa hasa wakati wa usajili”,alifafanua.

Aliwataka watu wanaoishi na maambukizi ya VVU watumie dawa kwa usahihi na kufuata miongozo wanayopewa na wataalamu wa afya.

“Dhumuni la Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais John Pombe Magufuli ni kutoa huduma nzuri kwa wananchi wake,tunaishukuru AGPAHI kwa kuendelea kushirikiana nasi katika mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI,tunahitaji Shinyanga isiyo na maambukizi mapya ya VVU”,alisema Dkt. Mlacha.

Kwa upande wao,Washiriki wa warsha hiyo waliahidi kutoa elimu zaidi kwa wateja kuhusu VVU na UKIMWI sambamba na kuwatafuta na kuwarudisha kwenye huduma wateja waliopotea.
Mratibu wa Kudhibiti na Kupambana na Ukimwi mkoa wa Shinyanga, Dkt. Peter Mlacha wakati akifunga warsha ya Watoa Huduma za VVU na UKIMWI mkoani Shinyanga katika ukumbi wa Virgimark Hotel Mjini Shinyanga - Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog
Mratibu wa Kudhibiti na Kupambana na Ukimwi mkoa wa Shinyanga, Dkt. Peter Mlacha akiwaomba watoa Huduma za VVU na UKIMWI kuongeza juhudi katika kufuatilia wateja waliopotea katika huduma.
Mratibu wa Huduma za VVU na UKIMWI katika jamii mkoa wa Shinyanga, Edwiga Zumba akizungumza wakati wa warsha hiyo.

Afisa Miradi Huduma Unganishi kwa Jamii AGPAHI mkoa wa  Shinyanga Nastervella Rweyemamu akizungumza wakati wa warsha hiyo.
Afisa Mawasiliano na Uraghbishi wa AGPAHI, Glory Macha akitoa neno la shukrani kwa washiriki wa warsha hiyo na kuwasisitiza kufanyia kazi mambo yote waliyojifunza kwa muda wa siku tatu kwenye warsha.


Washiriki wa warsha hiyo wakijaza fomu ya ufuatiliaji wa wateja kwenye vituo vya tiba na matunzo (CTC).
Watoa huduma za VVU na UKIMWI wakiendelea kujaza fomu.
Watoa huduma za VVU na UKIMWI wakisoma maelekezo kwenye fomu za ufuatiliaji.
Wawezeshaji wakati wa warsha hiyo wakiwa ukumbini.Kushoto ni Mwezeshaji wa Huduma za VVU na UKIMWI katika jamii Manispaa ya Shinyanga, Mwita Thomas na Mratibu wa Huduma za VVU na UKIMWI katika jamii mkoa wa Shinyanga, Edwiga Zumba.
Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527