WAZIRI AMPA SIKU 7 MKUU WA UPELELEZI ,SAKATA LA MWANAMKE KUCHOMEWA NYUMBA

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, ametoa siku saba kwa Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Mkoa wa Kagera (RCO), Obassy Nguvillan, kupeleleza upya kesi ya mama aliyechomewa nyumba katika eneo la Kyakailabwa Kata ya Nyanga, Manispaa ya Bukoba.

Lugola alitoa agizo hilo jana kutokana na watuhumiwa kukamatwa kisha kuachiwa na baadaye jalada kufungwa na Mwanasheria wa Serikali.

Kabla ya agizo hilo, mama huyo, Sauda Amir, alilalamika kwa Waziri Lugola katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika uwanja wa Uhuru Manispaa ya Bukoba na baadaye RCO alikiri kuwa inawezekana Jeshi la Polisi lilipeleleza kesi hiyo kwa udhaifu.

Lugola alisema kuwa haiwezekani mwanamke huyo achomewe nyumba, watuhumiwa anawafahamu halafu kesi iishe katika mazingira ambayo yana utata na kulazimika kumwita RCO kujibu.

“RCO natoa muda wa wiki moja ufanye kazi hii wewe mwenyewe, uchunguze kesi hii upya na unipe majibu,” alisema.

Akizungumzia tukio hilo, Sauda anayedai alifiwa na mumewe, alisema kuwa nyumba yake ilichomwa moto Juni 11, mwaka jana na kuwa kutokana na tukio hilo, kwa sasa hana mahala pa kuishi.

“Mheshimiwa Waziri, naomba unisaidie suala langu lipatiwe ufumbuzi, nahangaika na watoto, sina pa kuishi, kwa sasa mimi na watoto wangu saba tumepewa hifadhi na mama mmoja katika eneo la Kyakailabwa,” Alisema mama huyo

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527