WAZIRI LUKUVI ATOA HATI MILIKI ZA KIMILA KWA WANANCHI WA KIJIJI CHA MAPOGOLO

 Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi akitoa hati kwa mmoja ya mwananchi wa kijiji cha Mapogolo wilaya ya Iringa mkoani Iringa.
Baadhi ya wananchi wa kijiji cha Mapogolo waliohudhulia mkutano wa kutoa hati miliki.

 Na Fredy Mgunda- Iringa

NA FREDY MGUNDA,IRINGA

ZAIDI ya Kaya 200 za wafugaji wa kabila la Wamasai na Wamang’ati wamemilikishwa ardhi katika kijiji cha Mapogolo wilayani Iringa, hatua iliyoelezwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi kwamba “itamaliza migogoro ya wakulima na wafugaji na kukuza utanzania.”

Kaya hizo zilikabidhiwa hatimiliki za ardhi za kimila juzi katika hafla iliyohusisha ugawaji wa jumla ya hati 2,404 za mashamba kwa wananchi wa kijiji hicho kinachopakana na Hifadhi ya Taifa ya Ruaha.

Hati hizo zimetolewa kupitia mradi wa Urasimajishaji Ardhi Vijijini (LTA) unaotekelezwa kupitia  mpango wa Kupunguza Njaa na Utapiamlo (Feed The Future) kwa ufadhili wa Shirika la Maendeleo ya Kimataifa la Marekani (USAID).

“Leo tumeshuhudia makabila mbalimbali, wakiwemo ndugu zetu wamasai na wamang’ati wakipata ardhi katika ardhi ya wahehe. Hii ndio Tanzania, haina ubaguzi, mtu yoyote ana uwezo wa kufanya shughuli yoyote ya kimaendeleo mahali popote ili mradi havunji sheria,” alisema.

Alisema watanzania hawatarajii tena kusikia ugomvi baina ya wakulima na wafugaji katika kijiji hicho kwani mradi huo umeyawezesha makundi hayo kumiliki ardhi watakayoitumia kwa maendeleo yao endelevu katika jamii.

Mmoja wa wafugaji wa kabila la wamasai aliyemilikishwa ardhi katika kijiji hicho, Liwau Shang’ali aliwashukuru wenyeji wa kijiji hicho kwa kuikaribisha familia yake kijijini hapo akisema; “kama isingekuwa hivyo nisingewe kupata na kumiliki kisheria zaidi ya ekari saba za ardhi.”

Baada ya kupata shamba hilo, alisema hatarajii  kuepeleka mifugo yake kwenye mashamba ya watu wengine kwa kuwa shamba alilonalo linaweza kukidhi mahitaji ya mifugo yake kama ataliendeleza na kufuga kisasa baada ya kupata elimu.

Pamoja na kupata kipande hicho cha ardhi aliishukuru serikali ya kijiji kwa kupitia mradi huo kutenga eneo kubwa la malisho kwa ajili ya wafugaji akisema uamuzi huo unaongeza usalama wa mifugo yao, utalinda mashamba ya wakulima na hatimaye kukuza amani na ushirikiano miongoni mwao.

Awali Mkurugenzi wa LTA, Tressan Sulivan alisema mpango wa matumizi bora ya ardhi na upimaji ardhi una manufaa makubwa katika kupunguza umasikini na njaa katika jamii hasa za vijijini.

Alisema wakulima, wafugaji, wafanyabiashara, wanawake na wanaume wana haki ya kupata, kutumia, kumiliki na kugawa ardhi ili mradi wafuate sheria na taratibu zilizowekwa.

Sullivan alisema kwa kupitia mradi huo uelewa wa haki za wanawake na jamii katika kumiliki ardhi umeongezeka na umesaidia kuwahamasisha kutumia nafasi waliyopewa kuomba ardhi ambayo ni rasilimali muhimu katika kukuza kipato chao.

Katika kijiji hicho alisema mradi uliwezesha uandaaji wa mpango wa matumizi bora ya ardhi na kukarabati masijala ya ardhi na kutoa mafunzo juu ya haki za ardhi na matumizi ya rasilimali ardhi kiuzalishaji ili kuwawezesha wananchi kiuchumi.

Alisema waliopata hatimiliki za kimila wanaweza pia kuzitumia kama dhamana mahakamani na katika taasisi za fedha kupata mikopo itakayowawezesha kushughulikia changamoto walizonazo.

Alisema jumla ya vijiji 36 kati ya vijiji 133 vya wilaya hiyo vimenufaika na mradi huo ulioanza kutekelezwa mwaka 2015 na ambao utakamilika mwakani, 2019.

Mmoja wa wanawake walionufaika na mpango huo, Sakina Mlelwa alisema wanafurahi kuona mila na desturi zilizokuwa zikiwanyima haki ya kumiliki ardhi katika jamii zao zinapoteza nguvu zake mbele ya sheria mbalimbali za ardhi.  

“Tumeelimishwa jinsi sheria hizo zinavyoondoa tofauti za umiliki wa ardhi baina ya mwanamke na mwanaume, jamii inajua na imeanza kuuona umuhimu wa mwanamke kutobaguliwa katika umiliki wa ardhi,” Mlelwa alisema.

Alisema tatumia kipande chake cha ardhi chenye ukubwa wa heka tatu kutafuta mikopo atakayoitumia kuwekeza katika shughuli za kilimo na ufugaji.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527