WAHAMIAJI HARAMU 81 WANASWA DAR MSAKO SEHEMU ZA KAZI, NYUMBANI

Idara ya Uhamiaji Mkoa wa Dar es Salaam, imeanza kusaka wahamiaji haramu kwenye makazi na sehemu za kazi, ikiwamo kuwachukuliwa hatua za kisheria.


Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Kaimu Ofisa Uhamiaji Mkoa, Kamishna Mrakibu Mwandamizi wa Uhamiani, Novaita Mroso, alisema operesheni maalum imefanyika na inaendelea.

Alisema wameamua kuwasaka wahamiaji haramu kwenye mitaa, ili kuweza kuwadhibiti zaidi.

“Tukishindwa kukupata eneo la kazi tutakufuata nyumbani, kwa utaratibu tuliojiwekea Dar es Salaam, siyo sehemu salama kuwa maficho kwa wahamiaji haramu. Yeyote anayeajiri raia wa kigeni ahakikishe ana vibali vyote vya kuishi nchini,” alisema.

Alisema ilianza Januari 17 mwaka huu, na hadi jana ilikuwa na siku tano na jumla ya wahamiaji 81, ambao wanatuhumiwa kwa makosa mbalimbali walitiwa mbaroni.

“Kati yao tumebaini 35 wanatoka nchini Burundi, waliobaki wanatoka Somalia na Congo, wengine 46 wanaendelea kuchunguzwa na baada ya kukamilika tutabaini uhalali wao wa kuwapo nchini,” alisema.


Mroso alisema waliobainika kuwa ni wahamiaji haramu watachukuliwa hatua za kuwafikisha mahakamani na kuwafukuza nchini.


“Operesheni maalum ni sehemu ya jukumu letu la udhibiti wa wahamiaji haramu. Pia tumekuwa tukifanya uhakiki wa taarifa za wageni waliopo Mkoa wa Dar es Salaam ambao wamejiajiri au kuajiriwa,” alisema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527