TPDC YAFUNGUA MILANGO YA USHIRIKIANO NA ZPDC


Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) Mhandisi Kapuulya Musomba (kushoto) akipokea zawadi ya mlango kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Zanzibar (ZPDC) ikiwa ni ishara ya kufungua milango ya ushirikiano baina ya TPDC na ZPDC.
Viongozi mbalimbali wa TPDC na ZPDC wakifuatilia kwa makini maelezo yanayotolewa na Juvent Ndege (pipeline shift supervisor) katika kituo cha Kinyerezi jijini Dar es Salaam.
 **
Hivi karibuni Shirika la Maendeleo ya Petroli Zanzibar (ZPDC) lilifanya ziara yake ya kwanza kutembelea Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) na kufanya mazungumzo yenye lengo la kufungua milango ya ushirikiano baina ya mashirika haya ya mafuta na gesi hapa nchini. Hayo yalibainishwa na Mkurugenzi Mtendaji wa ZPDC Bi. Mwanamkaa Abdulrahman Mohamed.

Katika historia fupi ya ZPDC iliyosomwa na Bi Mwanamkaa Mohamed, alisema na kusisitiza kuwa ZPDC bado ni changa na hivyo basi kupitia ushirikiano huo wanahitaji kujifunza mengi na kufanya kazi kwa bidii ili kufikia viwango ikiwa bado wapo kwenye maboresho ya mfumo wa shirika.

“Tumesema tuje na kitu cha kuonyesha alama ya kufungua milango ya ushirikiano” alisema Bi Mwanamkaa huku akikabidhi alama ya mlango ikiwa ni ishara ya kufungua milango ya ushirikiano.

Naye Meneja mipango wa TPDC Lwaga Kibona aliungana na viongozi hao wa Zanzibar pamoja na wataalamu wa miradi ya gesi katika kutembelea miradi mbalimbali ya TPDC ikiwemo inayosambaza gesi asilia kwa matumizi ya viwandani, majumbani pamoja na kituo cha kujaza gesi kwenye magari (CNG) cha Ubungo na kituo cha kupokea gesi asilia Kinyerezi.

Katika kituo cha kupokelea gesi cha Kinyerezi, Mhandisi Baltazari Thomas ambaye ni Kaimu Meneja Mkuu wa kampuni tanzu ya TPDC ijulikanayo kama GASCO alifafanua mambo mbalimbali yanayohusiana na gesi asilia ikiwemo upatikanaji wake na jinsi inavyopokelewa na kusambazwa kwa wateja mbalimbali ikiwemo Tanesco kwa ajili ya kuzalisha umeme. Baada ya kupokea maelezo hayo waliungana na wataalamu wengine kutembelea eneo hili kujionea namna kazi zinavyofanyika.
Ujumbe kutoka Zanzibar ulionekana kuwa na maswali mengi yote yakiwa na lengo la kuwaongezea uelewa katika sekta hii ya mafuta na gesi pamoja na usimamizi wake.

Kupitia wataalam wabobezi wa TPDC wageni hawa walipata fursa ya kujifunza na kujiongezea uelewa ambapo mwishoni kabisa walilishukuru shirika kwa maelezo ambayo wameyatoa na kuweka ahadi ya kwenda kuwajibika katika njia hizo hizo na zaidi ili kuleta manufaa kwa nchi.

--

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527